Raia wanne kutoka                  China, jana walipandishwa katika kizimba cha Mahakama ya                  Hakimu Mkazi Mkoa wa Mbeya kujibu mashtaka matatu ya                  uhujumu uchumi likiwamo la kukutwa na pembe kumi na moja                  za faru zenye thamani ya Sh 902.8milioni.
                            Mwendesha mashtaka wa                  Serikali, Achiles Mulisa akisaidiana na Simon Wankyo,                  alidai kuwa washtakiwa wote kwa pamoja walishiriki                  kuhujumu uchumi kinyume cha sheria ya nchi.
              Pia, alidai kuwa                  walipanga njama na kutekeleza kuingiza nchini pembe hizo                  za faru bila kibali cha Serikali ya Tanzania na Umoja wa                  Mataifa, kwa kumiliki nyara hizo bila kibali.
              Mulisa alidai kuwa                  washtakiwa walikamatwa Novemba 6, mwaka huu katika mpaka                  wa Kasumulu wilayani Kyela wakiwa wamezificha pembe hizo                  kwenye gari walilokuwa wakisafiria kutoka nchini Malawi                  kuja Tanzania.
              Hata hivyo, washtakiwa                  wote walikana mashtaka na Wakili Mulisa alisema                  upelelezi wa shauri hilo umekamilika.
              Alimuomba Hakimu Mkazi                  Mfawidhi wa Mkoa, Michael Mteite apange tarehe ya                  kuendelea kusikilizwa kesi hiyo.
              Wakili wa upande wa                  utetezi, Ladslaus Lwekaza aliiomba mahakama iwapatie                  dhamana wateja wake kwa madai kwamba mashtaka                  wanayokabiliwa nayo yanatoa fursa ya kuwapo kwa dhamana                  hiyo. Hoja hiyo ilipingwa na mawakili wa Jamhuri,                  waliodai kuwa Mkurugenzi wa mashtaka amezuia dhamana.
              Mteite alikubaliana na                  hoja ya upande wa mashtaka ya kuzuia dhamana kwa                  washtakiwa hao na aliamuru warudishwe mahabusu. Kesi                  hiyo itaendelea leo na itasikilizwa kwa mfululizo siku                  mbili. 
MWANANCHI.
                
                
            MWANANCHI.
0 comments:
Post a Comment