Siku moja baada ya Rais John Magufuli na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kuwasimamisha watendaji wa Bandari na TRA, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue amemtaka kila mtendaji mkuu au ofisa masuhuli wa Serikali kujiuliza ni kwa kiasi gani anatekeleza kwa vitendo dhamira ya Rais ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima.
Alitoa kauli hiyo jana              katika taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano              Ikulu, ikifafanua maagizo ya Rais kuhusu kupunguza matumizi              yasiyo ya lazima katika wizara, idara na taasisi za              Serikali.
          Juzi, Majaliwa alifanya              ziara ya ghafla katika ofisi za Bandari na kuwasimamisha              watumishi hao akiwamo Kamishna wa Kodi na Forodha wa TRA,              Tiagi Masamaki na Habibu Mponezya wa Kitengo cha Huduma kwa              Wateja ambao wanatuhumiwa kwa ubadhirifu wa fedha uliotokana              na upotevu wa makontena zaidi ya 349.
          Baadaye, Rais Magufuli              alimsimamisha kazi Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade baada              ya kubaini 'madudu' katika ofisi za mamlaka hiyo ikiwa ni              mwendelezo wa kasi aliyoanza nayo katika ukaguzi na udhibiti              wa matumizi ya fedha za umma.
          "Rais ameonyesha njia, sasa              kwa wakati huu ni vyema kila mtendaji mkuu wa Serikali,              ajiulize endapo Rais Magufuli atafika katika eneo langu la              kazi, ni kwa kiasi gani atakuta nimetekeleza maagizo yake?"              alisema Balozi Sefue.
          Balozi Sefue pia              alizungumzia uchapishaji wa kalenda na vitabu vya kumbukumbu              huku akihoji umuhimu wa wake.
          "Kila mtendaji mkuu wa              Serikali au afisa masuhuli apime mwenyewe kama ni lazima              kutengeneza na kuchapisha kalenga na diary na kama ni lazima              achapishe kwa kiasi gani?
          "Ni matumizi mabaya ya              fedha za umma kwa kila wizara, idara na taasisi za Serikali              kuchapisha idadi kubwa ya kalenda na diaries ambazo wakati              mwingine hata hazitumiki mpaka mwaka unakwisha," aliongeza              Balozi Sefue.
          Kwa hatua zinazochukuliwa              ni dhahiri watendaji wakuu wa mashirika, taasisi za umma na              wizara mbalimbali watakuwa matumbo joto kwa kuwa hawajui ni              lini viongozi hao watatua kwao.
          Hayo yanatokea wakati              ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG)              iliyotolewa mapema mwaka huu inaonyesha ukaguzi uliofanywa              katika taasisi 176 za Serikali Kuu, halmashauri 163 na              mashirika ya umma 109 ulibaini ufisadi katika mishahara hewa              na katika miradi ya maendeleo.
          Mashirika ya umma              yanayotazamwa ni Shirika la Nyumba (NHC), Shirika la              Maendeleo ya Taifa (NDC), Shirika la Maendeleo ya Mafuta              (TPDC), Kampuni la Reli Tanzania (TRL), Shirika la Reli              Tanzania na Zambia (Tazara), Tanesco, mifuko ya hifadhi ya              jamii; NSSF, PPF, LAPF, PSPF, GEPF, NHIF na mashirika ya              hifadhi za taifa kama Tanapa na Ngorongoro pamoja na mamlaka              za udhibiti kama Ewura, Sumatra, TCRA, TCAA na SSRA.
          Kutokana na hatua hizo za              Rais Magufuli na Majaliwa, Waziri Mkuu wa zamani, Dk Salim              Ahmed Salim alisema kasi hiyo inawathibitishia Watanzania              kuwa alichokuwa akikisema Dk Magufuli na kukiahidi kipindi              cha kampeni ni cha kweli.
          Alisema hayo wakati              akizungumza na mwandishi wetu baada ya kufungua mahafali ya              13 ya Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki (HKMU),              yaliyofanyika, Dar es Salaam jana.
          "Watumishi wa Serikali hivi              sasa wajizatiti kufanya kazi kwa ufanisi na weledi ili              waendane na kasi hii ya Dk Magufuli.
          "Nina imani hata hawa              wauguzi na madaktari waliohitimu leo (jana), ambao wamepikwa              na kuiva, wataweza kuendana na kasi hii," alisema Dk Salim              ambaye pia ni mkuu wa chuo hicho.
          Watendaji wazungumza
Baadhi ya watendaji wa              mashirika ya umma waliozungumza jana kwa nyakati tofauti              walisema wako tayari kwenda sambamba na kasi ya Rais              Magufuli huku wengine wakiahidi kuzungumzia hilo siku tano              zijazo.
          Mkurugenzi Mtendaji wa              Tanesco, Mhandisi Felchesmi Mramba alisema Tanesco              imejiandaa kufanya kazi na Magufuli kwa kasi aliyoanza nayo.
          Alipoulizwa atawezaje              kwenda sambamba na kasi ya Rais Magufuli katikati ya shirika              linalokabiliwa na changamoto nyingi, Mramba alisita kutoa              ufafanuzi wa swali hilo kuahidi kulitolea majibu hivi              karibuni.
          Shirika hilo la umeme              limekuwa likikabiliwa na changamoto ya uchakavu wa              miundombinu ya usambazaji wa umeme, mikataba mibovu kwa              kampuni zinazouza umeme, kushindwa kukusanya fedha za mauzo              ya umeme na uhujumu na mitandao ya wizi wa umeme.
          Alipoulizwa, Msemaji wa              Tazara, Conrad Simuchile alitaka atumiwe maswali kwa mtandao              ili aweze kujibu kesho kupitia kwa Mkurugenzi Mtendaji,              Ronald Phiri.
          Januari mwaka huu, Phiri              aliliambia gazeti hili kuwa mamlaka hiyo inaweza kufa endapo              nchi washirika hazitawekeza mtaji mkubwa ili kuongeza              uzalishaji.Tazara imekuwa na migogoro ya muda mrefu na              wafanyakazi wake katika malipo ya mishahara lakini uongozi              wake unadai hali hiyo inachagizwa na kushuka kwa uzalishaji.              Kuhusu mpango wa kwenda na kasi ya Rais Magufuli ndani ya              TRL, Mkuu wa Masoko, Charles Ndenge alisema atatoa ufafanuzi              kesho ofisini kwake.
          Mei mwaka huu, aliyekuwa              Waziri wa uchukuzi, Samuel Sitta aliwasimamisha kazi vigogo              watano akiwamo Mkurugenzi Mtendaji TRL, Kipallo Kisamfu na              watumishi wengine wanne baada ya kupitia uchunguzi wa tuhuma              zilizowakabili.
          Watendaji hao              walisimamishwa kazi kutokana na tuhuma za kuhujumu mamlaka              hiyo kupitia ununuzi wa mabehewa mabovu 274 ya mizigo,              uliofanyika chini ya mkataba kati ya TRL na Kampuni ya M/S              Hindusthan, hatua iliyosababisha hasara ya Sh230 bilioni.
MWANANCHI.
        MWANANCHI.
0 comments:
Post a Comment