November 14, 2015

  • MGONJWA ALIYETIBIWA NA RAIS MAGUFULI KUFANYIWA UPASUAJI WIKI IJAYO



    MGONJWA ALIYETIBIWA NA RAIS MAGUFULI KUFANYIWA UPASUAJI WIKI IJAYO
    Rais Magufuli akisalimiana na mgonjwa Chacha


     Mgonjwa aliyeahidiwa matibabu na Rais John Magufuli, Chacha Makenge amefanyiwa uchunguzi na majibu ya kipimo cha MRI na sasa anasubiri upasuaji katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
    Chacha aliyekuwa amekwama kupatiwa matibabu kwa kukosekana vipimo vya CT Scan na MRI, amepatiwa matibabu hayo kwenye hospitali hiyo ya rufani chini ya uangalizi wa madaktari bingwa.
    Akizungumza na gazeti hili jana, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Taasisi ya Mifupa Muhimbili (Moi), Almas Jumaa alisema, Chacha alikuwa mgonjwa wa kwanza kufanyiwa kipimo cha MRI baada ya kutengamaa Novemba 11, amegundulika kuwa na tatizo kwenye uti wa mgongo.
    Alisema, awali mgonjwa huyo alifanyiwa kipimo cha CT Scan nje ya hospitali hiyo na kugundulika ana matatizo kadhaa, lakini MNH ilihitaji kujiridhisha na ndipo walipogundua mvunjiko katika pingili zake za uti wa mgongo.
    " Kwa sasa, anaendelea vizuri na baada ya vipimo madaktari wamegundua katika uti wake wa mgongo kuna mahali kulikuwa na mvunjiko na inavyoonyesha aliupata muda mrefu, alikuwa akiishi na tatizo hilo, madaktari wameshauri wiki ijayo afanyiwe upasuaji ili kurekebisha tatizo hilo," alisema Almas.
    Alipotembelewa katika wodi ya Sewahaji, Chacha aliyelazwa hospitalini hapo Septemba 8, alisema tangu Rais Magufuli afanye ziara yake, wamekuwa wakitibiwa kwa wakati kutokana na mashine hiyo kurekebishwa.
    "Nimpe pole na pongezi rais kwa kazi ngumu aliyoifanya, ameunganisha daraja baina ya MNH na Moi, awali ilikuwa ngumu, lakini sasa kuna urahisi wa huduma, matengenezo ya vipimo yameokoa wagonjwa wengi.
    "Awali, kupata vipimo nje ilichukua muda ili kukamilika," alisema Chacha, aliyedai alisubiri vipimo vya MRI na CT Scan kwa miezi miwili.
    Alipoulizwa hali halisi ya kipimo cha CT Scan, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Muhimbili, Aminiel Aligaesha alisema bado mafundi kutoka Kampuni ya Phillips ya Uholanzi wanaendelea na matengenezo ya mashine hiyo.
    "Kipimo cha CT Scan bado kipo kwenye matengenezo na pindi kitakapotengamaa tutaufahamisha umma na kwa kuwa wanaotengeneza wanatokea Kampuni ya Muccos, itakapokuwa imeleta shida watakuja mafundi kutoka Uholanzi," alisema Aligaesha.
    Novemba 9, Rais Magufuli alifanya ziara ya kushtukiza MNH na kukutana na kasoro lukuki, zikiwamo za wagonjwa kulala sakafuni, mashine za vipimo na uchunguzi wa magonjwa kutofaya kazi kwa zaidi ya miezi miwili.


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.