HAPA kazi tu! Zile ziara za              kushtukiza (bila taarifa) zinazofanywa na Rais wa Awamu ya              Tano wa Jamhuri ya Muungano za Tanzania, Dk. John Pombe              Magufuli 'JPM' zimezua kizaazaa mjini hapa, hususan katika              Mahakama ya Mwanzo ya Morogoro.
          Katika safishasafisha hiyo, baadhi ya            makarani walivaa kanga kwa kujifunga juu ya magauni yao kama            wapo majumbani mwao kwa lengo la kujikinga na vumbi la muda            mrefu ndani ya mashelfu ya mafaili mahakamani hapo.
          Karani wa mahakama hiyo            aliyejitambulisha kwa jina la Mwajuma Nyundo alipoulizwa na            paparazi wetu kuhusu zoezi la usafi huo, alisema:
          "Hapa ni kizaazaa tu! Si unaona kasi ya            Rais Magufuli ya sapraizi akitekeleza kauli mbiu yake ya 'Hapa            Kazi Tu'. Hivyo katika kutekeleza kauli mbiu hiyo leo viongozi            wetu wametupa kazi hii."
          Akizungumza na gazeti hili kwa sharti la            kutotajwa jina gazetini, mfanyakazi mwingine alisema lengo la            kuweka ofisi katika hali ya usafi ni kuhofia kuumbuka endapo            Magufuli atatia timu ghafla.
          "Si unajua Magufuli anavyotikisa nchi            kwa sasa. Yaani huwezi kujua muda wala saa atakayoibukia            kwako. Tumeamua kufanya usafi ili mahakama iwe safi.
          "Sasa hivi hata zile kesi za muda mrefu            tunapanga mafaili upya, yakae mbelembele na kuweka lebo ya            kutamabulisha kesi ili mashauri hayo yaendelee na kumalizika            kwa wakati," alisema mfanyakazi huyo huku akiendelea na            shughuli zake.
          Mfanyakazi mwingine naye alisema:            "Tunatekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya Rais Magufuli ya 'Hapa            Kazi Tu' ili akifanya ziara ya ghafla katika mahakama yetu            atukute tuko vizuri."
          Baada ya kusikia hayo kutoka kwa            wafanyakazi wa mahakama hiyo, paparazi wetu alibisha hodi            kwenye mlango wa chumba cha mashtaka na kuzungumza na kiongozi            wa mahakama hiyo, Mheshimiwa Janne Melle ambapo alipoulizwa            alisema:
          "Na mimi nimepokea maagizo haya kutoka            Mahakama ya Wilaya. Halafu bwana mwandishi hizo picha            ulizopiga naomba sana ukishazisafisha niletee na mimi            nizipeleke wilayani."
          KUMBE SI MAHAKAMANI TU
          Ukiachia mahakama hiyo, wafanyakazi            wengi wa ofisi za serikali mkoani hapa wamebadili tabia ambapo            sasa, saa moja asubuhi wapo barabarani kwa lengo la kuwahi            muda wa kuingia kazini ambao ni saa moja na nusu tofauti na            zamani ambazo kuchelewa kazini ilionekana kama fasheni.
          WASEMAVYO MOROGORO
          Baadhi ya wakazi wa mjini hapa            walipoongea na Ijumaa kuhusu tabia ya            Magufuli ya kuzuka maofisini bila taarifa, walipongeza huku            wakisema huyo ndiye rais anayetakiwa kwa sasa hapa Bongo.
          "Tabia zetu Wabongo tunataka rais kama            Magufuli. Unajua sisi ni watu wa kusukumwa sana! Sasa            tukimpata rais asiyeweza kusukuma, ndiyo nchi inakwenda mrama.            Mimi nampongeza sana Magufuli.
          "Kwa staili hii ya Magufuli ya            kushtukiza ziara ya maeneo mbalimbali watu watanyooka. Kwa            wale wavivu na wazembe makazini lazima waombe po," alisema            Jumanne Kihamba, mkazi wa Misufini mjini hapa.
          GUMZO LA NCHI NI MAGUFULI
          Kwa sasa ukiachia vyombo vya habari kama            magazeti, ndani ya mitandao mbalimbali ya kijamii gumzo ni            Magufuli. Hiyo yote ni kufuatia hatua yake ya kufanya ziara za            kushtukiza ambapo tangu aingie madarakani ameshawashtukiza            watumishi wa Wizara ya Fedha (Hazina) na Hospitali ya Taifa            Muhimbili (MNH).
          Kitendo hicho kimeibua mpaka utani            kwenye mitandao ambapo baadhi ya watu wamekuwa wakitunga            vituko mbalimbali kuashiria kwamba, Magufuli ni kiboko ya            watendaji wazembe serikalini.
        
0 comments:
Post a Comment