November 14, 2015

  • Ratiba ya Uchaguzi wa Spika wa Bunge Pamoja na Uteuzi wa Waziri Mkuu


    Ratiba ya Uchaguzi wa Spika wa Bunge Pamoja na Uteuzi wa Waziri Mkuu
    Spika  wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anatarajiwa kuchaguliwa mjini Dodoma Jumanne ijayo, ratiba ya Bunge hilo imeeleza.
     
    Kutokana na ratiba hiyo, ni wazi Chama Cha Mapinduzi (CCM), kitalazimika kumtaja mgombea wake atakayekuwa na nafasi kubwa ya kuwa Spika kati ya kesho na keshokutwa na kumaliza mvutano wa nani anafaa kuwa spika, baada ya wanachama 22 kujitokeza mpaka jana kuwania nafasi hiyo.

    "Kutokana na kuitishwa kwa Bunge na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dk John Pombe Joseph Magufuli... Ofisi ya Bunge inapenda kuwatangazia wabunge wateule wote kuwa wanatakiwa kuwasili mjini Dodoma Novemba 13, 2015 (jana) tayari kwa ajili ya usajili utakalofanyika bungeni kuanzia siku hiyo hiyo," imeeleza ratiba hiyo iliyowekwa katika ukurasa wa Facebook wa Bunge.

    Kwa mujibu wa ratiba hiyo, kuanzia jana mpaka kesho, wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, watapaswa kuwa wameshawasili mjini Dodoma na kujisajili kwa watumishi wa Bunge ambao wameshaanza kazi hiyo.

    Baada ya kazi hiyo, ratiba ya Bunge hilo imeonesha kuwa keshokutwa siku ya Jumatatu, wabunge wote wanatarajiwa wawe wameshajisajili ili saa nne asubuhi washiriki kikao cha maelekezo katika Ukumbi wa Bunge kitakachohusisha kutembelea ukumbi huo.

    Ratiba hiyo inaonesha kuwa siku hiyo hiyo kuanzia saa 10 jioni, wabunge hao watakuwa na mikutano ya vyama vyao, ambako inatarajiwa hoja kubwa itakuwa jina la Spika na Naibu Spika.

    Spika
    Siku ya Jumanne wiki ijayo, Watanzania wataelekeza macho yao na masikio katika Kikao cha Kwanza cha Bunge la 11 mkoani hapa, ambacho kitatanguliwa na kusomwa kwa tamko la Rais Magufuli la kuitisha Bunge.

    Mara baada ya kusomwa kwa tamko hilo, kutafuatiwa na uchaguzi wa Spika utakaofanyika kwa kura za siri na mshindi akishatangazwa, atakula kiapo siku hiyo hiyo, kisha atapigiwa Wimbo wa Taifa na dua itasomwa.

    Siku hiyo hiyo, Spika huyo anatarajiwa kuanza kuapisha wabunge na kazi hiyo ataendelea nayo siku ya Jumatano na kumalizia siku ya Alhamisi asubuhi kwa wabunge watakaokuwa hawajala kiapo cha uaminifu.

    Waziri Mkuu, Naibu Spika
    Alhamisi ya Novemba 19, saa 10 jioni Rais Magufuli anatarajiwa kupeleka kwa Spika jina la Waziri Mkuu ambalo litasomwa mbele ya wabunge wote na kuthibitishwa na wabunge kwa kura.

    Baada ya kuthibitishwa kwa Waziri Mkuu, siku hiyo hiyo Naibu Spika atachaguliwa na kula kiapo cha uaminifu na baada ya hapo wabunge watajiweka tayari kwa Hotuba ya Kwanza ya Rais Magufuli itakayotolewa Ijumaa saa kumi jioni na kufuatiwa na kuahirishwa kwa Bunge.

  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.