November 26, 2015

  • MAHAKAMA YA MAFISADI MAMBO YAIVA,MCHAKATO WAANZA RASMI


    MAHAKAMA YA MAFISADI MAMBO YAIVA,MCHAKATO WAANZA RASMI

     Jaji Kiongozi, Shaban                    Lila       Utekelezaji wa ahadi za Rais John Magufuli unazidi kushika kasi baada ya kuanza kwa mchakato wa kuanzisha mahakama maalumu ya kuwashughulikia mafisadi.
    Jaji Kiongozi, Shaban Lila alisema jana kuwa tayari wadau mbalimbali wa haki jinai wameanza kukutana kuangalia namna ya kuanzisha mahakama hiyo kama sehemu ya utekejezaji wa ahadi ya Rais.
    Akizungumza katika hafla ya kuhitimisha mafunzo ya kushughulikia mashauri nyeti ya jinai kwa majaji 12 wa Mahakama Kuu ya Tanzania, alisema juzi walikuwa na mazungumzo na Wizara ya Katiba na Sheria kuangalia mfumo wa uendeshaji wa mahakama hiyo.
    "Tunaangalia tuianzishe kama mahakama huru au ifanywe ndani ya muundo wetu wa mahakama kwa kuipa kipaumbele maalumu. Lakini tunafikiria zaidi kama ingekuwa ni kitengo maalumu ndani ya Mahakama Kuu kitakachokuwa kikishughulikia mafisadi," alisema Jaji Lila.
    Hata hivyo, Jaji Lila hakutaja muda maalumu utakaotumika kumaliza mchakato wa kuanzisha mahakama hiyo, huku akisema unahusisha wadau wengi na unyeti wake unahitaji maandalizi makubwa.
    Jaji huyo bila kutaja takwimu, alieleza kuwa kesi za makosa makubwa ya jinai zinaongezeka nchini ukilinganisha na miaka ya nyuma hasa zile zinazohusu utakatishaji fedha, ugaidi, usafirishaji wa dawa za kulevya, usafirishaji wa nyara za Serikali hasa wanyama hai na mazao yake na ufisadi.
    Balozi wa Uingereza nchini, Dianna Melrose alimpongeza Rais Magufuli kwa kuonyesha msimamo wa kupambana na makosa ya jinai yakiwamo ya dawa ya kulevya, usafirishaji wa nyara za Serikali na utakatishaji fedha.
    "Nilikuwa nimeketi bungeni namsikiliza Rais siku alipokuwa akilihutubia Bunge, japo hotuba yake ilikuwa kwa Kiswahili lakini nilipata faraja kubwa nilipomuona akiwa mkali katika masuala hayo," alisema Balozi Melrose.     


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.