May 17, 2014

  • MAJANGA: WAZAZI WASUSA MAITI YA MTOTO WAO


    Haijakaa sawa! Tofauti na desturi ya Kitanzania watu kuwa pamoja katika kipindi cha matatizo, wazazi wa marehemu, Leonard Jorome Mwakanyamale, wanadaiwa kususa kuzika maiti ya mtoto wao kisa ugomvi kati ya marehemu na nduguze.
    Kijana Leonard Jorome Mwakanyamale,enzi za uhai wake
    Leonard ambaye alikuwa akiishi Buguruni jijini Dar, alifariki dunia Mei 10, mwaka huu kwa Ugonjwa wa Malaria.

    Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa jirani mmoja ambaye hakutaka jina lichorwe , Leonard alikuwa na ugomvi na familia yake na aliapa kutokanyaga kwao mkoani Mbeya tangu alipokwenda kumzika bibi yake, zaidi ya miaka mitano iliyopita.
    "Tangu nijuane na Leonard zaidi ya mwaka wa tano, hajakanyaga kwao.
    "Nilisikia mara ya mwisho kwenda kwao ilikuwa msiba wa bibi yake.
    "Tunasikia wakati anatoka Mbeya kuna maneno yaliwakera wazazi wake, inawezekana ndiyo yamewachefua na kushindwa kumsamehe kwani nasikia alidai hatarudi tena Mbeya kwa kuwa watu aliokuwa akiwapenda walishamalizika, yaani bibi yake.
    Mwili wa Leonard Jorome Mwakanyamale,ukiwa makabulini tayali kwa mazishi
    "Sijui kwa nini alisema maneno hayo japokuwa uwezo wa kumsafirisha ulikuwepo kabisa lakini wazazi walikataa asipelekwe kwa kuwa alipasusa kwao hivyo azikwe Dar es Salaam na siyo mkoani Mbeya," alisema jirani huyo.
    Jitihada za kuwatafuta ndugu wa marehemu ziligonga mwamba kwani simu zao hazikuwa hewani, kupitia habari hii wakiisoma, wanaweza kutoa ufafanuzi.
    Naye mke wa marehemu, Letisia Mbilite hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo kwani alikuwa haamini kilichotokea na alikuwa na majonzi mazito.
    Baada ya wazazi kutokubali kushiriki mazishi ya mtoto wao, marafiki waliungana, wakauhifadhi mwili katika Hospitali ya Amana, Dar kisha kusomewa misa na Mwenyekiti wa Kanisa la Parokia ya Stephano, Shahidi Anton Makala na kuzikwa katika Makaburi ya Wailes yaliyopo Chang'ombe, Dar.
  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.