May 29, 2014

  • Je Kwa Mwanamke Ndoa Ndiyo Kila Kitu?

    Katika makuzi yangu kama binti wa Kiafrika nimefunzwa mambo mengi kuhusu maisha na wajibu wangu kama mtoto wa kike.

    Baada ya kuvunja ungo nilianza kuandaliwa kuwa mke mtarajiwa wa mwanaume nisiyemfahamu. 

    Nimefunzwa kupika, nimefunzwa usafi wangu wa mwili, nimefunzwa usafi wa nyumba, nimefunzwa kuvumilia maisha ya ndoa na nikaaminishwa kwamba mwanaume ndiye kichwa cha nyumba na nikafunzwa wajibu wangu katika kumtumikia, lakini pia nikafunzwa kupanga bajeti na kuweka akiba ili huyu mume ambaye ni kichwa cha nyumba akikwama kupata mkate wa kila siku kwa ajili ya familia niweze kumsaidia.

    Kwa kifupi ni kwamba nilifunzwa mambo mengi lakini yote hayo yakiniaminisha kwamba siku isiyo na jina lazima nitaolewa na kuwa chini ya mwanaume ambaye atakuwa ndiye kila kitu kwangu.

    Nakumbuka wakati fulani baada ya mama kuona mabinti ambao nalingana nao umri na wengine nikiwa nimewazidi umri wakiolewa pale mtaani mama alianza kunidodosa kama sijapata mtu kama wenzangu.

    Lakini pia alijaribu kutumia misamiati mbalimbali na mafumbo lakini nilielewa kwamba alikuwa anamaanisha nisiwe mgumu sana kwa wanaume kwani sijui aliyevutiwa na mimi na anayetaka kunioa. 

    Nadhani alikuwa anataka kufikisha ujumbe kuwa umri unasonga na wenzangu wanaolewambona miye sisomeki?

    Naamini si mimi peke yangu, ninayekabiliana na changamoto hizi za wazazi na jamii kwa ujumla.

    Ukweli ni kwamba malezi ya mtoto wa kike yanamuandaa kuwa mke wa mtu, yanamuandaa kuolewa na yanamuaminisha kwamba ndoa ndiyo kila kitu.
  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.