May 27, 2014

  • Msama ampongeza Mwakyembe kuifufua ATCL

    Mkurugenzi wa Msama Promotins Alex Msama (kulia),  akiwa na Mratibu wa Tamasha la Pasaka John Melele, wakifurahia kusafiri na Jet 103 ndege ya ATCL hivi karibuni

    SERIKALI kupitia Wizara ya Uchukuzi inayoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe inastahili, pongezi kwa kupiga hatua kubwa kujenga na kuimarisha sekta ya usafirishaji wa anga nchini.

    Mkurugenzi wa Msama Promotins Alex Msama, ametoa pongezi hizo siku chache baada ya Wizara hiyo kuendelea kuonesha mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za anga nchini.

    Msama ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu amewahimiza Watanzania kujawa na uzalendo na hivyo, kuliunga mkono Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kwa kutumia huduma zake zilizoboreshwa ili liweze kupambana na changamoto  mbalimbali zilizopo katika sekta ya usafirishaji wa anga nchini.

    Alisema hatua ya Wizara ya Uchukuzi kuwekeza katika usafiri wa anga inapaswa kuungwa mkono na kila Mtanzania kwa maslahi ya taifa.

    “Huduma zinazotolewa na ATCL sasa ni nzuri na zenye ubora unaolingana na mazingira ya sasa, hivyo ni vema sisi Watanzania tujivunie; kila Mtanzania anapaswa kujivunia na kutumia huduma za shirika hilo.” 

    Hata hivyo, alitoa rai kwa makampuni, taasisi zote za serikali na mtu mmoja mmoja kutumia ndege ya shirika hilo linalofanya safari zake katika mikoa mbalimbali nchini. Kwamba hatua pekee ya kuongeza ufanisi wa ATCL ni watu kutumia  chao na kukilinda na kukituza.

    Mpaka sasa ATCL ina ndege mbili ikiwamo ya Jet 103, ambazo kwa muda mfupi, zimeonesha ufanisi wa hali ya juu katika utoaji huduma wa safari za anga.

    Aliongeza kuwa amefurahishwa na huduma ya Ndege ya ATCL itokayo Dar kwenda Mwanza ambapo alisema kuwa ndege hiyo ni nzuri na pia huduma zake ni nzuri na ikiwa angani inatulia mpaka unajisahau kama upo ndani ya ndege.

    Aidha alisema kuwa ni vyema kila mtanzania akatumia ndege hii kwani kwa ndege zote alizopanda kwenda Mwanza hii ni ndege bora zaidi.

    Pia amewaasa Watanzania kuwa wazalendo kama wenzetu wakenya ambao wamekuwa wazelendo kwa kutumia ndege zao kila wafanyapo safari, na hivyo ni vema watanzania  kutumia ndege za ATCL ili kusaidia shirika hilo kutoka ndege mbili hadi kuongeza ndege zaidi.
  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.