May 17, 2014

  • Serikali yashikwa pabaya bungeni

     
     
     
     
    Dodoma/Dar es Salaam. Kashfa ya zaidi ya Sh200 bilioni za Akaunti ya Escrow ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imechukua sura mpya baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema kudai kuwapo kwa watu wanaonunua mashahidi.

    Jaji Werema alitoa kauli hiyo nzito bungeni mjini Dodoma juzi, kauli ambayo imeibua maswali mengi kuliko majibu, kuhusu ni nani wanaotoa fedha kutafuta mashahidi na kwa masilahi ya nani hasa.

    "Ninafahamu kwamba kuna watu wengi wanatumia fedha kwa ajili ya kutafuta mashahidi, lakini haituhusu, palipo na haki, haki itasimama na haki ya mtu haipotei," alisema Werema katika kauli inayoonyesha kukata tamaa.

    Werema alitoa wito kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuendelea na uchunguzi na waufanye haraka na kwa umakini.

    "Uamuzi uliofanyika hapa ni kwamba uchunguzi uendelee na vyombo vilivyoteuliwa ni Takukuru na CAG na bado vinafanya uchunguzi… Nahimiza vyombo hivyo vifanye kazi hiyo haraka na kwa umakini," alisema.

    Hata hivyo, Werema alitahadharisha kuwa ni vyema ikafahamika, akaunti ya Escrow ilianzishwa kwa malengo maalumu. Akaunti hiyo ilifunguliwa na Kampuni ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

    Werema alikiri zipo kodi ikiwamo ya Ongezeko la Thamani (VAT), ambayo ilipaswa kulipwa na Tanesco na kodi ya Manufaa (capital gain) inapaswa kulipwa na Kampuni iliyoiuza IPTL kwa Pan African Power Ltd (PAP).

    Wiki iliyopita, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema hoja iliyopo na inayoleta ubishani ni kuondoa fedha katika akaunti ya Escrow na kuzipeleka.

    Waziri Mkuu alisema: "Kwa tuhuma zenyewe zilivyo itabidi tuwahusishe Takukuru nao wafanye kazi kwa upande wao ili kupata ukweli kwa sababu wako pia viongozi wa Serikali wanaotuhumiwa katika suala hilo, hivyo ni vyema likachunguzwa kwa uzito wake ili wale watakaobainika wamekula rushwa washtakiwe.

    Kadhalika Waziri Mkuu aliliomba Bunge limruhusu CAG kukamilisha kazi hiyo.
  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.