May 26, 2014

  • UKAWA:Tusipobembelezwa Haturudi Bungeni



    Ukawa:Tusipobembelezwa Haturudi Bungeni
    Viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) wakiwa wanaendelea kufanya mikutano ya hadhara nchi nzima kudai Katiba ya wananchi, bado viongozi hao wanasisitiza kwamba kamwe hawatarudi kwenye Bunge la Malaamu la Katiba kama njia za kistaarabu za kuwaomba warudi hazitatumika.

    Kabla ya kuanza kuzunguka mikoani, Ukawa walianza kampeni za kudai Katiba inayotokana na maoni ya wananchi kupitia Bunge Maalumu la Katiba.

    Ukawa wanapinga mchakato huo kutekwa na CCM, kwa madai kuwa wamekuwa wakitumia wingi wao ndani ya Bunge hilo kuchakachua maoni yaliyotolewa na wananchi kupitia Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

    Ziara za viongozi hao wa Ukawa mikoani, zina lengo la kuunganisha nguvu za kudai Katiba ya Wananchi na kuwashirikisha wananchi kuhusu kinachofanywa bungeni.

    Vyama vinavyounda Ukawa ambavyo viongozi wake wakuu wanazunguka mikoani ni Katibu Mkuu wa Chadema Dk Willibrod Slaa, Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba na Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi Mosena Nyambambe.

    Baadhi ya madai ya Ukawa yanayozungumzwa katika ziara hizo ni mwenendo wa Bunge Maalumu la Katiba na kutekwa kwa wanasiasa kutoka chama kilicho na wajumbe wengi ndani ya Bunge Maalumu la Katiba.

    Wakati Ukawa wakiendelea na ratiba zao za kuzunguka mikoani, Bunge Maalumu la Katiba limesimama kwa muda hadi mwezi Agosti kupisha Bunge la Bajeti ambalo linaendelea mjini Dodoma.

    Wenje awasha moto Mwanza

    Mbunge wa Nyamagana kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Ezekia Wenje, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya fedha ya Ukawa, anasema kuwa hawatarudi kwenye Bunge la Katiba kama njia za kistaarabu hazitatumika kuwaomba warudi.

    Wenje alitoa kauli hiyo alipokuwa akiwahutubia mamia ya wakazi wa Jiji la Mwanza katika viwanja vya Dampo mkoani humo.

    Akishangiliwa na umati huo wa watu, Wenje anasema Ukawa wataendelea kudai Katiba ya Wananchi hadi pale itakapopatikana. "Kutokana na mapambano yangu bungeni sasa jina limebadilika. Najulikana Jenero na siyo mtoto wa mama ntilie tena na kwa kudhihirisha hilo nitahakikisha maoni ya wananchi hayachakachuliwi na Katiba itakayopatikana itakuwa ya wananchi wote," anasema.

    "Nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) namtaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda atumie njia za kistaarabu na kuonyesha ustaarabu katika kutusihi turudi kwenye Bunge Maalumu la Katiba mwezi Agosti la sivyo, hatutarejea ng'o," anasema

    Anasema kama watakwenda kinyume na kutumia njia wanazozitaka wao ili warudi kwenye Bunge Maalumu la Katiba, wao wataendelea na msimamo wao hadi hapo Katiba ya wananchi itakapopatikana.

    Amshukia Kinana

    Katika hatua nyingine mbunge huyo wa Nyamagana amewataka wananchi kuwapuuza viongozi wa CCM wanaopita na kupiga propaganda kwamba katiba haina faida kwao.

    Kuna watu wanapita na kuwadanganya kuwa katiba haina faida kwenu kwa kuwa haiwezi kuwaletea chakula. Hizo ni propaganda zipuuzeni, anasema.

    Anasema anashangaa kusikia kwamba Katiba haiwezi kuwasaidia wananchi kupata chakula, kwani huo ni uzushi wa kisiasa na kwamba Watanzania wasisikilize maneno ya wanasiasa hao.

    Wenje anaeleza kuwa Watanzania wa leo siyo kama wa miaka iliyopita, kwani wengi wao wamesoma na wanajua mambo hivyo huwezi kuwadanganya kwa propaganda za kisiasa.

    Mchakato ulivurugikia Ikulu

    Wenje anasema "Naomba niwaambie ndugu zangu wa Mwanza, kwamba mchakato wa Mabadiliko ya Katiba, ulivurugwa tangu hatua za uteuzi wa wajumbe wa kundi la wajumbe 201 waliyoteuliwa na Rais Jakaya Kikwete, kwani idadi hiyo ni kubwa na imejaa makada wa CCM."

    Anaendelea "Kazi inayofanywa na baadhi ya wajumbe walioteuliwa na Rais Kikwete ni kutetea mambo wanayotaka CCM, jambo ambalo siyo jema, kwani Katiba siyo ya CCM ni mali ya Watanzania wote."



  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.