WAZIRI wa Nishati na            Madini, George Simbachawene amesema zipo dalili njema za            kugundua gesi katika maeneo mengine nchini baada ya            kugundulika kwa gesi asilia futi za ujazo trilioni 55.08            katika mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani.
        Simbachawene alitaja            maeneo ambayo yameonesha dalili ya kuwepo gesi asilia mbali na            mikoa ya Lindi na Mtwara kuwa ni Morogoro na Pangani . Alisema            hayo hivi karibuni Makao Makuu ya Wizara, wakati akitoa            nyaraka za ufadhili wa masomo kwa Watanzania 22 waliopata            ufadhili kusomea masuala ya mafuta na gesi katika ngazi za            Shahada za Uzamivu na Uzamili , nchini China.
        Alisema kuwa, uwepo wa            gesi asilia katika mikoa ya Lindi na Mtwara na dalili ambazo            zimeonekana katika maeneo mengine ni kiashiria kuwa, Tanzania            inaingia katika uchumi wa gesi . Alisema taifa linatarajiwa            kunufaika na rasilimali hiyo kwa kuwa kiwango kilichopatikana            ni kikubwa cha kuifanya nchi kupiga hatua kubwa kimaendeleo            kupitia rasilimali hiyo.
        "Kuna nchi zina gesi futi            za ujazo 10 tu lakini wamepiga hatua kubwa ya maendeleo            kupitia gesi asilia. Kwa kiasi tulichonacho na ambacho            tunaendelea kugundua ni wazi kuwa tunaingia katika uchumi wa            gesi na ndio sababu tumeanza kutayarisha wataalamu wetu            wenyewe," aliongeza Simbachawene.
        Akizungumzia Sheria            zilizosainiwa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete, alisema            zinaondoa wasiwasi wa namna taifa litakavyonufaika na            rasilimali hiyo. Sheria hizo ni Sheria ya Mafuta na Gesi            Asilia, Uwazi na Uwajibikaji na Sheria ya Usimamizi wa Mapato            ya Mafuta na Gesi Asilia
        
0 comments:
Post a Comment