KITUO            cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeitaka Sekretarieti            ya Maadili ya Viongozi wa Umma, kutoa orodha ya viongozi wa            umma wanaogombea nafasi mbalimbali katika Uchaguzi Mkuu, ambao            walishahojiwa na kuwekwa hatiani kutokana na maadili yao.
        Chombo            hicho kimetakiwa kutowafumbia macho viongozi wanaowania            nyadhifa mbalimbali ambao walishindwa kuonesha kiwango cha juu            cha maadili wakati wa uongozi wao au wakati wakiwa katika            nyadhifa walizowahi kushika.
        Mkurugenzi            Mtendaji wa LHRC, Dk Hellen Kijo Bisimba alisema hayo jana Dar            es Salaam, wakati akizungumzia maadili ya viongozi wa umma            wakati Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imeshabariki kuanza            rasmi kwa kampeni za kuwania nafasi hizo.
        "Katika            kipindi hiki tumeshuhudia vyama vya siasa vikipitisha viongozi            kuwania nyadhifa mbalimbali na katika michakato mbalimbali ya            vyama na kuonesha viashiria vya kutoheshimu misingi ya            maadili," alisema Dk Bisimba.
        Alisema            baadhi ya walioteuliwa wameshahusishwa, kutajwa na kushitakiwa            katika vyombo vya kisheria na vya kikatiba kwa tuhuma za utovu            wa maadili.
        Alizitaja            kashfa hizo kuwa ni rushwa, matumizi mabaya ya ofisi za umma            na kutowajibika, vitendo ambavyo ni kinyume na misingi ya            Katiba, sheria na ahadi ya uadilifu ambayo kiongozi wa umma            kwa mujibu wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma namba 13            ya mwaka 1995 kifungu cha 6.
        Dk            Bisimba alisema sheria hiyo inamtaka kiongozi wa umma kuwa mtu            atakayekuwa na kiwango cha juu cha maadili kadri iwezekanavyo,            ili wananchi kuwa na imani na kutotiliwa shaka katika uadilifu            wake.
        Ameitaka            Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kutopitisha majina ya            wagombea waliopendekezwa na vyama mbalimbali, ambao            walishatuhumiwa au kushitakiwa kwa kashfa za rushwa,            kujilimbikizia mali na matumizi mabaya ya ofisi za umma.
        Kwa            misingi hiyo, Dk Bisimba pia ameisisitiza sekretarieti iweke            wazi majina ya viongozi wa umma ambao hawajatoa taarifa kuhusu            mali walizonazo kwa mujibu wa sheria.
        Aidha,            ameitaka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) kwa            kuzingatia Sheria za Kupambana na Kudhibiti Rushwa na Sheria            ya Gharama za Uchaguzi, kuweka na kusimamia mkakati            utakaodhibiti mianya ya rushwa na matumizi yasiyo halali ya            fedha katika kampeni hizo.
        *Polisi
        Katika            hatua nyingine, Jeshi la Polisi nchini limetaka vyama vyote            vyenye vikundi vya ulinzi vyenye mwelekeo wa kijeshi, kuvunja            vikundi hivyo mara moja kwa kuwa vimekuwa vikiingilia majukumu            ya jeshi hilo jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
        Kamishna            wa Polisi Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja alisema hayo            alipozungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Makao            Makuu ya jeshi hilo, Jijini Dar es Salaam.
        Alitaja            vikundi hiyo kuwa ni pamoja na Green Guard, Red Brigade na            Blue Guard ambapo alisema kuendelea kumiliki vikundi hivyo kwa            kisingizio chochote, ni uvunjifu wa Katiba ya nchi na Sheria            ya Vyama vya Siasa, jambo ambalo jeshi hilo haliwezi            kuvumiliana.
        "Hatua            stahiki za kisheria zitachukuliwa kwa chama chochote            kitakachoendelea kukaidi amri hii," alisema Changonja. Pia            alisema katika kipindi hiki cha kampeni, ni muhimu kila mmoja            ajiepushe na makosa yanayoweza kusababisha jinai.
        "Mfano            wa baadhi ya makosa hayo ni pamoja na kutokutoa taarifa kwa            Jeshi la Polisi ndani ya muda ulioruhusiwa kisheria ambao ni            saa 48 kabla ya mkutano wa kampeni kuanza, kufanya kampeni            kabla au baada ya muda ulioruhusiwa, kutumia lugha ya matusi            na kashfa kwa wagombea wengine.
        "Kueneza            uongo dhidi ya mgombea wa chama kingine, kuondoa, kuchana au            kubandua matangazo ya wagombea. Kuandika maneno mengine katika            matangazo yaliyobandikwa, kuzuia watu wengine kusoma matangazo            hayo au kubandika tangazo katika maeneo yaliyozuiliwa au juu            ya tangazo lingine," alisema Kamishna huyo.
        Chagonja            alikumbusha wagombea wote kwa nafasi zao kuelimisha wafuasi            wao umuhimu wa kuheshimu sheria, ili kudumisha amani, usalama            na utulivu katika kipindi chote cha mchakato wa uchaguzi.
        Alisema            jeshi hilo limejipanga vizuri kuhakikisha mikutano yote ya            kampeni inafanyika katika hali ya amani na utulivu hadi siku            ya uchaguzi na uwepo wa Polisi katika kampeni hizo unalenga            kuzuia uhalifu na sio kudhoofisha kampeni, hivyo wananchi            watoe ushirikiano kwa jeshi hilo kwa kutii sheria bila            shuruti.
        Kutokana            na hali hiyo Jeshi la Polisi limetoa tahadhari kwa wananchi            wote na vyama vyote vya siasa, kuzingatia sheria            zinazowaongoza, ikiwemo sheria ya vyama vya siasa na miongozo            mbalimbali ambayo imekuwa ikitolewa na Mwenyekiti wa Tume ya            Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian Lubuva.
        Alisema            lengo ni kuhakikisha kipindi chote cha kampeni hadi Uchaguzi            Mkuu, kila moja anajiepusha na vitendo vyenye mwelekeo wa            uvunjifu wa sheria.
        
0 comments:
Post a Comment