August 22, 2015

  • Serikali yakabidhiwa nyaraka za umiliki wa General Tyre...sasa iko chini ya serikali



    Serikali yakabidhiwa nyaraka za umiliki wa General Tyre...sasa iko chini ya serikali

    Hatimaye serikali imekabidhiwa rasmi hati ya hisa na nyaraka muhimu za ununuzi wa asilimia 26 zilizokuwa zikimilikiwa na General Tyre International Company (GTIC).

    Hatua hiyo inaifanya serikali kuimiliki kampuni hiyo kwa asilimia 100, makabidhiano hayo yalifanyika jijini Dar es Salaam jana na kushuhudiwa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue.

    Balozi Sefue alisema kiwanda hicho, ambachio kilianzishwa nchini mwaka 1969 kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania (ambayo ilimiliki asilimia 74 ya hisa zote) na kampuni ya General Tyre International Company ya Marekani (iliyokuwa na hisa asilimia 26), kilikuwa kinazalisha na kuuza matairi  320,000 kwa mwaka.

    Alisema lengo la serikali ni kufufua kiwanda hicho na kuanza kuzalisha matairi yenye ubora ambayo yatahimiri ushindani katika soko la ndani na ukanda wa Afrika Mashariki, na akasisitiza kuwa NDC inaendelea kutayarisha mazingira bora ya uwekezaji ili kuwavutia wawekezaji watakaoshirikiana nao katika kukamilisha kufufua.

    Sefue alisema wataalamu wanaendelea kufanya tathmini ya kiufundi inayohusisha ukaguzi wa mashine, mitambo pamoja na miundombinu ya kiwanda, ili kujua ukubwa wa kazi na kiasi cha fedha kitakachohitajika katika kufufua mitambo hiyo.

    Alitoa pongezi kwa Rais Jakaya Kikwete kuwa katika nyakati mbali mbali, Rais alionyesha kuguswa na hali ya kiwanda hicho na kila mara alikuwa akihimiza jitihada za kufufua kiwanda hicho zifanyike haraka na kwamba angependa kuona hatua za kufufua kiwanda hicho zimekamilika hata kabla hajastaafu u-rais

    Katibu Mkuu wa Viwanda na Biashara, Uledi Mussa alisema kiwanda cha General Tyre ni muhimu kwa uchumi wa taifa, na pia kwa wananchi wa Arusha kutokana na ajira pamoja na biashara za matairi yatakayozaloshwa katika kiwanda hicho.

    Mwakilishi wa kampuni ya Continental Arktiengesellschaft Germany (Continental AG), Chapple Thomas ambaye alikabidhi hati ya hisa na nyaraka nyingine kwa niaba ya kampuni hiyo, aliishukuru serikali ya Tanzania kwa ushirikiano pamoja na makubaliano waliyoyafanya na hatimaye kubadilishana hati za makubaliano hayo kisheria.       



  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.