POLISI mkoani Morogoro wanashikilia watu 11, wakazi wa Kijiji cha Mpofu wilayani Kilombero kwa tuhuma za kuvamia na kuchoma moto kituo kidogo cha polisi na ofisi ya serikali ya kijiji hicho.
Watuhumiwa hao ni sehemu ya zaidi              ya watu 100 wanaodaiwa kufanya uhalifu huo katika kituo              hicho cha polisi Mbingu, katika taarifa ya Mgeta.
        Watuhumiwa hao wanadaiwa kufanya              tukio hilo wakishinikiza polisi wamwachie mtuhumiwa              aliyewekwa mahabusu katika kituo hicho, Bashiri Kadugula              (25), kwa tuhuma za kumshambulia mkewe, Veronica Chabula              (21) ili wamwadhibu.
        Kamanda wa Polisi wa mkoa wa              Morogoro, Leonard Paulo, alisema jana kuwa, Kadugula              aliwekwa ndani kwa kumkata mkewe kwa panga sehemu mbalimbali              za mwili kutokana na wivu wa mapenzi.
        Alisema katika tukio hilo ni la              Agosti 20, mwaka huu saa 4:00 usiku, mtuhumiwa huyo baada ya              kufanya kitendo hicho kwa mkewe akitoroka na ndugu wa              Veronica walifanikiwa kumkamata na kumfikisha kituo kidogo              cha Polisi Mbingu, ili hatua za kisheria zichukuliwe.
        Alisema baada ya ndugu kuondoka              kituo cha polisi, kitambo kidogo kulitokea kundi la watu              wakirusha mawe kituoni hapo, wakitaka wamuue mtuhumiwa huyo              kwa kukerwa na kitendo chake cha kinyama. Kamanda Paulo              alisema, askari waliokuwepo kituoni hapo walijitahidi              kuwazuia watu hao lakini walizidiwa nguvu.
        Alisema polisi walifanikiwa              kumtoa mtuhumiwa mahabusu na kumwokoa sambamba na kuokoa              silaha za kituo hicho.
        Alisema, watu hao waliokadiriwa              kuwa zaidi ya 100, walivamia kituo hicho kidogo cha Polisi              na kukichoma moto ambapo nyaraka mbalimbali zilizokuwa ndani              ya kituo hicho ziliungua na kuteketea kabisa.
        Kamanda wa Polisi wa mkoa              alivitaja vitu vilivyoteketea kwa moto kuwa ni pamoja na              pikipiki tano zenye usajili T 979 BGA aina ya Sky Mark, T901              BUJ aina ya Sanlug, T801 BQA aina ya Sanlug, mali ya Askari              Wilson, T194 BVR aina ya T-Better, mali ya Askari Isaya na              T904 BUJ aina ya Tianda.
        Alisema, kundi la watu hao baada              ya kukichoma moto kituo kidogo cha polisi, lilivamia pia              Ofisi ya Serikali ya Kijiji cha Mpofu na kisha kuchoma moto              nyaraka mbalimbali, ambapo katika matukio hayo watuhumiwa 11              walikamatwa.
        Amewataja waliokamatwa kutokana              na tukio hilo kuwa ni Imani Mwampombe (40), Geofrey              Mwaikambo (46), Eugen Kikoti (41), Janken Mwaikambo (55),              Meshack Kikoti (42), Eliud Chumbula (52) na Shukrani Lukimo              (35) ambao ni wakulima na wakazi wa kijiji hicho cha Mpofu.
        Wengine waliokamatwa ni madereva              wawili wa bodaboda ambao ni Ramadhani Hussein (29), mkazi wa              Kitongoji cha Ngajengwana, Salum Ngala (36), John Mtikila              (55) na Rodrick Mwaikambo (36) wote wakulima na wakazi wa              Kijiji cha Tandale- Igima.
        Kamanda huyo wa Polisi wa mkoa              alisema kwamba watuhumiwa hao wanaendelea kuhojiwa na              watafikishwa mahakamani mara upelelezi utakapokamilika na              kwamba polisi wanaendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine              waliotoroka na kusisitiza kuwa wananchi wanapaswa kutii              sheria na kuacha kujichukulia sheria mkononi.
        
0 comments:
Post a Comment