VITUO vya maarifa sita            vitakavyotoa huduma za afya vinatarajiwa kujengwa kando ya            barabara kunusuru madereva wa masafa marefu kutoka Dar es            Salaam hadi Tunduru. Meneja Mradi wa North Star Alliance            anayeratibu ujenzi huo, Edger Mapunda alisema jana alipokuwa            akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
        Mapunda alisema            wanatambua sekta ya usafirishaji inakabiliwa na changamoto ya            masuala ya Ukimwi hivyo wameona kuna sababu ya kuwasaidia            madereva kwa kuwa wawapo safarini wanakutana na watu            mbalimbali. Alisema ujenzi wa vituo hivyo utakapokamilika            utawanufaisha pia wananchi waliopo jirani na vituo hivyo.
        Pia watatoa elimu ya            afya, upimaji wa magonjwa mbalimbali ikiwemo kisukari pamoja            na uendeshaji salama kwa madereva wawapo barabarani. Alisema            vituo viwili vitajengwa katika jiji la Dar es Salaam eneo la            bandarini, vingine viwili vitajengwa katika mkoa wa Iringa na            viwili vitajengwa mkoani Mbeya.
        "Maambukizi ni makubwa            katika maeneo hayo. Tulifanya tafiti tokea mwaka 2013            tukagundua mkusanyiko ni mkubwa katika maeneo hayo. Pia            Tunduma na Iringa tuligundua huduma za afya sio nyingi,"            alisema.
        Alisema gharama za mradi            mzima ni dola za Marekani milioni moja, na kwamba vituo kama            hivyo vimejengwa pia katika nchi ya Kenya ambapo vipo tisa,            Afrika Kusini vipo 12 na Malawi viwili.
        Mkurugenzi wa Uraghibishi            na Habari Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (Tacaids), Jumanne            Issango alisema wamekuwa na mkutano wa kujadili uanzishwaji wa            mradi wa kujenga vituo sita vya maarifa kandokando ya barabara            kuanzia Dar es Salaam hadi Tunduru.
        Alisema mradi huo utakuwa            wa miaka mitatu ulianza Aprili mwaka huu na kumalizika mwaka            2018. Mwakilishi wa madereva wanaosafiri masafa marefu kutoka            Chama cha Madereva nchini, Mohamed Sharrif alisema amekuwa na            wasiwasi na mradi kama huo unapomalizika huduma zinazokuwepo            zinadumaa kwa kukosa mfadhili.
        
0 comments:
Post a Comment