Wauguzi            wakiwa katika wodi iliyotengwa kwa ajili ya kuwahudumia            wagonjwa wenye dalili za kipindupindu katika Hospitali ya            Mwananyamala, Dar es Salaam, jana. Picha na Salim Shao 
        Dar es Salaam. Ugonjwa wa              kipindupindu umeingia Dar es Salaam na kusababisha watu              wawili kupoteza maisha na wengine 26 kulazwa katika              hospitali za Mwananyamala na Sinza.
          Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya              Kinondoni, Mhandisi Musa Nati alisema watu wengine wa nne              wamethibitika kuugua kipindupindu na waliolazwa katika              hospitali hizo wameonekana kuwa na dalili za ugonjwa huo.
        Alisema wodi mbili zimetengwa              katika hospitali hizo kwa ajili ya wagonjwa wenye dalili              hizo.
        Mkurugenzi huyo alisema kwa sasa              wanaandaa kambi maalumu kwa ajili ya wagonjwa wa              kipindupindu katika eneo la Mburahati.
        Alisema wameanza kuchukua              tahadhari kwa kupuliza dawa katika maeneo yaliyoripotiwa              kuwa na mlipuko wa ugonjwa huo.
        "Maeneo tuliyopuliza dawa ni              Manzese, Tandale na vitongoji vya Kijitonyama katika Wilaya              ya Kinondoni," alisema Nati
        Awali, Mganga Mkuu wa Wilaya ya              Kinondoni, Aziz Msuya alisema mmoja wa wagonjwa alifariki              dunia wakati akipelekwa Hospitali ya Mwananyamala na              mwingine alipoteza maisha akiwa nyumbani na mwili wake              kupelekwa Hospitali ya Sinza kuhifadhiwa.
        Alisema katika kuchukua tahadhari              ofisi yake imetoa dawa za kunywa na za kupulizia kwa kaya 70              katika maeneo ya Kijitonyama, Mtaa wa Ali Maua.
        Dk Msuya aliwataka wananchi              kuchukua tahadhari pale wanapoona mgonjwa anakuwa na dalili              za ugonjwa huo ili wamuwahishe katika kituo cha afya. Pia,              aliwataka kuhakikisha wananawa mikono kila wakati wanapotoka              msalani au kusalimiana kwa kushikana mikono.
        "Tumeshawasiliana na wenzetu wa              Bohari ya Dawa (MSD) ili kuhakikisha tunakuwa na dawa za              kutosha."
        Mganga Mkuu wa Hospitali ya              Mwananyamala, Sophinias Ngonyani alisema wagonjwa              waliothibitika kuwa na kipindupindu ni wawili na wengine 11              bado sampuli zao ziko maabara.
        Alisema wagonjwa hao wanaendelea              kupatiwa huduma wakiwa katika wodi maalumu iliyotengwa huku              wakisubiri majibu.
        Alipoulizwa juu ya hatua              zilizochukuliwa kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa huo, Mkuu              wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda alitupa mpira kwa Mkuu              wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik ambaye naye              alisema bado hajapewa taarifa kuhusu kuwapo kwa ugonjwa huo.
        
0 comments:
Post a Comment