June 19, 2014

  • WAZIRI MAGHEMBE ATOA MSIMAMO WA TANZANIA KUHUSU MTO NILE



    WAZIRI MAGHEMBE ATOA MSIMAMO WA TANZANIA KUHUSU MTO NILE
    Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe akiwa na mgeni wake, Balozi, Dk. Yassir Mohammed Ali, ofisini kwake pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Kuratibu Programu Ya Maji, Joseph Kakunda.
    Waziri wa Maji akiagana na mgeni wake, Balozi, Dk. Yassir Mohammed Ali.

    Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe jana alikutana na Balozi wa Sudan Nchini, Dk. Yassir Mohammed Ali, ofisini kwake kwa ajili ya mazungumzo mafupi, hususani matumizi ya maji ya Mto Nile.

    Waziri Maghembe alisema Tanzania haina mpango wa kuharibu maji ya Mto Nile kama wengi wanavyofikiri, zaidi ya kutaka kuhakikisha hatua sahihi zinachukuliwa ili kutatua tatizo la kupungua kwa kina cha maji kutokana na matumizi ya kibinadamu kukithiri na hivyo kuhatarisha uwepo wa mto huo.

    "Tanzania inachangia asilimia 28 ya maji ya Mto Nile na inatumia kiasi kidogo sana cha maji hayo kwa matumizi yake kwa asilimia 0.072 tu, huku ujazo wa mto huo ukiwa ni mita za ujazo bil 89, kuna haja ya kupata uwiano mzuri wa matumizi ya maji hayo tofauti na ilivyo sasa.", alisema Prof. Maghembe.

    Prof. Maghembe alisisitiza msimamo wa Tanzania ni kuhakikisha matumizi mazuri na sahihi, utunzaji na ulinzi wa maji ya Mto Nile ili kuhakikisha upatikanaji wa maji ya kutosha kwa watu wote sasa na baadae. Huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano, na kuahidi Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano kwa Jumuiya hiyo na Afrika Mashariki na Kati ili kuhakikisha wananchi wananufaika ipasavyo na mto huo.

    Balozi, Dk. Yassir alisema amefurahishwa na mtazamo wa Tanzania kwa kuhakikisha utunzwaji na matumizi mazuri ya maji ya Mto Nile na kuipongeza kwa kutoa ushirikiano chanya katika kuleta maendeleo ya Sekta ya Maji Afrika Mashariki na Kati. Hivi karibuni, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alitoa tamko la Tanzania kuendelea na mazungumzo ya Mkataba wa Maji ya Mto Nile na kusema Tanzania haijapanga kujitoa katika mchakato huo, bali unategemea kupelekwa Bungeni mwezi Novemba kwa ajili ya kuujadili kabla ya kuupitisha.

    Waziri Maghembe leo yupo Sudan, jijini Khartoum katika Mkutano wa 22 wa Baraza la Mawaziri wa Maji (Nile-COM) unaofanyika leo.


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.