May 20, 2014

  • Wakala wa mbegu kutekeleza ahadi ya Rais ya kuzalisha mchele tani 1.5 milioni



    Na Nathaniel Limu, Babati
    WAKALA wa Mbegu za Kilimo wa Taifa (ASA) umejiwekea mikakati madhubuti ya kuhakikisha ifikapo mwaka 2015, uzalishaji wa mchele nchini uwe umefikia tani 1.5 milioni ili kutekeleza agizo alilotoa Rais Jakaya Kikwete.
    Hayo yamesemwa hivi karibuni na Meneja Masoko na Usambazaji ASA,Philemon Kawamala kwa nyakati tofauti wakati akikagua mashamba darasa ya mazao ya alizeti,mtama,uwele,mahindi,mpunga wa mabondeni na ule wa mpunga mpya ambao unalimwa kwenye ardhi ya nyanda za juu.
    Akifafanua,amesema mpunga huo mpya ambao unalimwa kwenye ardhi inayolimwa mazao mengine ya kawaida kama mahindi na uwele,ni new rice for Africa (NERICA),mbegu zake ni za aina ya Nerica 1,2,4 na 7, pia kuna aina nyingine ambayo ni WAB 450.
    “Kwa mara ya kwanza mpunga huo mpya umepandwa katika mikoa ya Dodoma,Morogoro,Singida,Manyara,Tabora,Simiyu.Kagera,Shinyanga na Geita.
    Aina hizi za mpunga zinapandwa katika maeneo ya nyanda za juu (nchi kavu) hususan maeneo yanayolimwa mazao kama mahindi”,alifafanua zaidi Kawamala.
    wakulima picsWakulima shambani
    Amesema ujio wa mpunga huo pamoja na mchele uliozoeleka wa mabondeni kwa vyovyote endapo hali ya hewa na mvua zitaendelea kunyesha vizuri basi agizo la Rais Kikwete la kutaka nchi kuzalisha tani 1.5 milioni mwakani litafikiwa na pengine na kuzidi hapo.
    Kawamala amesema pamoja na mbegu hizo za mpunga mpya,ASA ina aina nyingi za mbegu bora zikiwemo za mazao ya mahindi na mtama ambazo zinakomaa kwa muda mfupi na mazao yake ni mengi ilikilinganishwa na mbegu za asili.
    “Kwa sasa kwa kutumia mashamba darasa yanayosimamiwa na wakulima viongozi,wakulima wamepanda mbegu hizo kwa lengo la kuwapa fursa wakulima kuchagua aina ya mbegu watakazozipenda zaidi ili uzalishaji wake uongezwe kadri ya mahitaji yao”amesema na kuongeza;
    “Nimefarijika mno kuona wakulima viongozi wamefanya kazi nzuri msimu huu kwa mazao ya alizeti,mahindi,mpunga wa mabonde ya umwagiliaji,majaruba na huu mpya uliolimwa kwenye nyanda za juu”.
    Kwa upande wao wakulima viongozi,wameupongeza ASA, kwa madai kwamba mbegu zake zitasaidia kuondoa kabisa uhaba wa chakula na wakati huo huo kuongeza kipato cha mkulima.
    “Mbegu kutoka ASA zimeonyesha dhahiri zitasaidia Tanzania kujitosheleza kwa chakula na kwa sababu zinatoa mazao mengi ikilinganishwa na mbegu za asili,mazao ya ziada yatakayopatikana yatasaidia kumkomboa mkulima kiuchumi”,amesema mkulima kiongozi wa kijiji cha Orongadida kata ya Qash.

    Naye Simon Lohay wa kijiji cha Mwakantisi kata ya Mamire,amesema mpunga mpya unaolimwa kwenye ardhi isiyo na maji sambamba na mazao ya mtama na mahindi umevutia wakulima wengi na msimu ujao wakulima karibu wote wameonyesha nia ya kuulima.
  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.