KIKUNDI cha ngoma                  cha selo kilichopo katika kijiji cha Kweingoma, wilayani                  Handeni, mkoani Tanga, kimesema kimepania vikali Desemba                  13 mwaka huu kufanya balaa katika tamasha la Handeni                  Kwetu 2014, litakalofanyika wilayani hapa.
          Shauku ya kikundi                  hicho imetolewa na Kiongozi wao Zaina Selemani,                  alipozungumzia umuhimu wa tamasha hilo, ambalo mwaka                  jana walishindwa kushiriki kutokana na wasanii wake                  wengi kukabiliwa na mambo ya kifamilia, ikiwamo kuugua                  na kuuguliwa.
          Akizungumza kwa                  furaha kubwa, Zaina alisema ngoma ya selo ni nzuri                  inayoshawishi kuangalia wasanii wanapokuwa jukwaani,                  hivyo mashabiki na wadau wote watapata burudani nzuri.
          "Mwaka huu                  tutashiriki kwa nguvu zote kwasababu ni tamasha                  lililoanza vizuri kwa mkoa huu wa Tanga, maana vikundi                  vingi kutoka sehemu mbalimbali za Handeni na mkoa wa                  Tanga vinashiriki," alisema.
          Naye Mratibu Mkuu                  wa tamasha hilo, Kambi Mbwana, alisema kuwa kwa siku                  kadhaa walikuwa wakifanya ziara kadhaa katika vijiji                  ambavyo vina vikundi vya ngoma za asili ili vishiriki,                  hususan vile ambavyo mwaka jana havikushiriki.
          "Tunataka kuongeza                  wigo wa vikundi kutoka ndani ya Tanga na nje pia,                  ukizingatia kuwa tunahitaji tamasha lenye nguvu na mguso                  pia ili kukuza sekta ya utamaduni na uchumi wa nchi                  yetu," alisema Mbwana.
          Tamasha la Handeni                  Kwetu lililopangwa kufanyika Desemba 13 katika Uwanja wa                  Azimio (Kigoda Stadium), ni moja ya matukio makubwa                  mkoani Tanga yanayokutanisha mamia ya watu kutoka sehemu                  mbalimbali za Tanzania.
          
0 comments:
Post a Comment