| Frank Nyalusi, Mwenyekiti wa Chadema Iringa Mjini | 
CHAMA cha Demokrasia na                    Maendeleo (Chadema) jimbo la Iringa Mjini jana                    limeshindwa kufanya maandamano ya amani kama                    ilivyotangazwa kwa kile kilichoelezwa na Mwenyekiti                    wake, Frank Nyalusi "tumepokea zuio kali kutoka jeshi                    la Polisi."
                    Akizungumza Jana Nyalusi alisema                    walitoa taarifa kwa jeshi hilo siku mbili zilizopita                    wakielezea nia yao ya kufanya maandamano hayo ikiwa                    ni kuitikia wito uliotangazwa na Mwenyekiti                    wao wa Taifa, Freeman Mbowe wa kufanya maandamano ya                    amani yasio na ukomo yenye lengo la kushinikiza                    kusitishwa kwa Bunge la Katiba.
                    Alisema pamoja na jeshi hilo                    kuwazuia kufanya maandamano hayo, jana hiyo hiyo                    waliruhusiwa kufanya mkutano wa hadhara uliotarajiwa                    kufanyika mtaa wenye machinga wengi maarufu kama                    magari mabovu, Kitanzini.
                    "Kwahiyo tutakuwa na mkutano wa                    hadhara utakaohutubiwa na mimi mwenyewe na viongozi                    wengine wa chama kuanzia saa 10 jioni, hivisasa tupo                    kwenye kikao cha kamati tendaji kuweka maazimio kuhusu                    zuio la maandamano hayo ya amani" alisema kwa njia ya                    simu.
                    Akieleza kushangazwa na maamuzi                    ya Polisi ya kuzuia maandamano yao, Nyalusi alisema                    maazimio yatakayofikiwa katika kikao hicho                    atayatangaza kwenye mkutano huo.
                    Wakati Chadema wakidai                    kudhibitiwa kufanya maandamano hayo, Kamanda wa Polisi                    wa Mkoa wa Iringa, Ramadhani Mungi alisema jeshi hilo                    halijapokea barua yoyote kutoka katika chama hicho                    inayoonesha wameomba kufanya maandamano hayo.
                    Akitoa ufafanuzi huo kwa njia ya                    simu, Mungi alisema "nchi hii kama zilivyo nchi                    nyingine inaendeshwa kwa sheria, taratibu na kanuni."
                    Alisema watanzania bila kujali                    wanatoka kundi gani ni lazima wafanye mambo wanayotaka                    kufanya kwa kuzingatia sheria vinginevyo mkono wa                    sheria utawafukuzia.
                    Alisema mji wa Iringa upo shwari                    na kwamba jeshi la Polisi limejipanga kikamilifu                    kukabiliana na hali yoyote ile itakayoonekana inataka                    kuhatarisha amani.
                    Aliwataka wakazi wa Iringa                    kuendelea na shughuli zao kama kawaida na pale                    watakahisi au kusikia kuna mtu au kikundi chochote cha                    watu kinataka kufanya jambo linaloweza kuhatarisha                    usalama wao na wa mali zao, watoe ushirikiano kwa                    kutoa taarifa Polisi.
                    kwa hisani ya francis godwin                    blog
        
0 comments:
Post a Comment