SWADAKTA! Katika hali ya              kustaajabisha, kijana mmoja aliyefahamika kwa jina la              Ramadhan, ambaye mwishoni mwa wiki amejikuta akishushiwa              kipigo kwa kudhaniwa kuwa kibaka, alisalimika baada ya              kuanza kusali kwa kuwashtakia kwa Mwenyezi Mungu waliokuwa              wakimpiga, akisema hakuwa na hatia na ghafla watu hao              kusitisha kipigo.
                Ramadhan alikutana na hali hiyo              baada ya kutuhumiwa kuiba redio kutoka katika duka moja              lililopo stendi ya daladala mjini hapa.
        Ilidaiwa kuwa kibaka huyo baada              ya kuchukua redio hiyo alianza kukimbia kutokana na mwenye              duka kumwitia mwizi na Ramadhan akawa mmoja kati ya watu              waliokuwa wakimfukuza, kabla ya mdokozi huyo kujichanganya              na watu hivyo kutotambulika kirahisi.
        Baada ya kuona hivyo, wananchi              hao wenye hasira walimgeukia kijana huyo na kuanza kumpa              kipigo kama cha mbwa mwizi kwa vile nguo zake zilikuwa              zimefanana na zile zilizokuwa zimevaliwa na kibaka aliyekuwa              akifukuzwa.
        "Ewe                  Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, kwa msaada wako                  niepushie na mtihani huu niliosingiziwa kwani wewe ndiwe                  unayejua ukweli wa tukio hili," mtu huyo              alisikika akisema kufuatia kipigo alichokuwa akikipata,              baada ya kukimbia na kwenda kujibanza pembeni ya duka              linalouza vinywaji baridi.
        Kufuatia maneno hayo, watu wote              walijikuta wakisitisha zoezi la kumpiga na mmoja wa bodaboda              wa kijiwe cha Juwata aliingia kati na kusema; "Jamani huyu jamaa anaonekana                  siyo mwizi na ni mtu wa dini, hivyo naomba aliyeibiwa                  ajitokeze na kutoa ushuhuda," alisema na              hakuna aliyejitokeza.
        Baada ya kuona hivyo, kijana huyo              aliwataka watu hao kumuacha aende zake huku baadhi ya              walioshiriki kumpiga wakimuomba msamaha mtu huyo aliyekuwa              akivuja damu mwili mzima.Akizungumza na mwandishi wetu,              Ramadhan alisema alishuka kwenye daladala na kuungana na              watu waliokuwa wakimfukuza mwizi kabla hawajamgeuzia kibao              kutokana na nguo zake kufanana na za kibaka.
        "Mwizi                  alijichanganya na watu ndipo nikageukiwa mimi,                  nikakimbilia hapa dukani kwa Mhindi na kuamua kuomba                  msaada kwa Mungu kwa kuomba na akafanikiwa kuniokoa,"              alisema kijana huyo.
        Katika stendi ya daladala,              mfanyabiashara wa duka lililoibiwa, aliyejitambulisha kwa              jina la Shaaban, alisema alikuwa amekwenda kutafuta chenchi,              ndipo alipomuona mtu akiondoka na redio yake na yeye akapiga              kelele za mwizi, akadondosha bidhaa hiyo na kukimbia, lakini              akashindwa kuungana na watu kumkimbiza kwa vile hakukuwa na              mtu mwingine dukani.
        
0 comments:
Post a Comment