October 20, 2015

  • WENYE SIMU ZA WHATSAPP, BLOGGERS, VYOMBO VYA HABARI HII INAWAHUSU SIKU YA UCHAGUZI TCRA YATOA ONYO



    WENYE SIMU ZA WHATSAPP, BLOGGERS, VYOMBO VYA HABARI HII INAWAHUSU SIKU YA UCHAGUZI TCRA YATOA ONYO

    Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui na Maadili wa TCRA, Injinia Margaret Munyagi (katikati) akifafanua jambo
    MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imevionya vyombo vya habari vitakavyotangaza matokeo ya uchaguzi mkuu kinyume cha sheria na taratibu kwamba haitasita kuviadhibu. Anaandika Charles William … (endelea).
    Mbele ya wanahabari leo jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Kamati ya maudhui ya vyombo vya habari, Injinia Magreth Munyagi ameonya kuwa utangazaji wa matokeo ya uchaguzi kabla ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ambao umekuwa ukizungumzwa na baadhi ya wanasiasa lazima uzingatie taratibu zilizowekwa na tume tofauti na hapo hatua kali zitachukuliwa na TCRA.
    Kumekuwa na mvutano baina ya Tume na vyama vya upinzani hususani vile vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kuhusu utangazaji wa matokeo ya uchaguzi mkuu mwaka huu huku Tume ikisisitiza kuwa ndiyo yenye mamlaka ya kutangaza matokeo na vyama hivyo vikisema hakuna sheria inayovizuia kutangaza matokeo ya vyama vyao.
    Wiki tatu zilizopita, Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bara), John Mnyika alisema "hakuna sheria inayotuzuia kutangaza matokeo ya kura zetu na ndio maana tunasisitiza tutayatangaza matokeo yetu wenyewe iwapo tutamaliza kujumlisha kabla ya masaa 72 ambayo NEC inasema itakuwa imemaliza."
    Akijibu swali la MwanaHALISI Online iwapo vyombo vya habari kutangaza matokeo yatakayokuwa yametolewa na chama au vyama vya siasa ni kosa kisheria, Injinia Munyagi amesema "Tumeshaeleza kwamba utangazaji matokeo lazima uzingatie sheria na taratibu za NEC."
    Baadhi ya adhabu zilizotajwa kutumika kwa atakayethibitika amevunja sheria ni kuonywa, kupigwa faini, kufungiwa kwa muda na kunyang'anywa leseni ya utangazaji.
    Pia Mamlaka kupitia kamati hiyo ya maudhui ya vyombo vya habari, imeeleza kuridhishwa kwa 'wastani' na utolewaji wa matangazo ya habari za kampeni.
    "Mpaka sasa tumeridhishwa kwa wastani na kazi iliyofanywa na vyombo vya habari katika kampeni za uchaguzi mkuu, taarifa za uchochezi na kutia hofu zimepungua na waandishi wanajitahidi kutafuta vyanzo sahihi vya habari zao," ameeleza mwenyekiti injinia Munyagi.
    Kamati ya Maudhui huteuliwa kisheria na waziri mwenye dhamana ya masuala ya habari jukumu kubwa la kamati hiyo likiwa ni kufanya tathimini za mara kwa mara kuhusu maudhui ya utangazaji na kupokea maoni au malalamiko juu ya maudhui ya vipindi hivyo.


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.