October 13, 2015

  • MSAJILI -AWAASA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA KUHUSU AMANI



    MSAJILI -AWAASA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA KUHUSU AMANI
    2
    Msajili wa Vyama Vya Siasa, Jaji Francis Mutungi akizungumza na waandishi wa habari  Jumatatu Oktoba 12, 2015  kwenye ukumbi wa mikutano uliopo katika ofisi hiyo jijini Dares Salaam kuhusiana na masuala ya amani kuelekea Uchaguzi Mkuu na baada ya uchaguzi huo.


    Picha zote na Magreth Kinabo-Maelezo.
    3
    Msanii Mrisho Mpoto akizungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa mikutano uliopo katika ofisi hiyo jijini Dares Salaam kuhusiana na masuala ya amani kuelekea Uchaguzi Mkuu na baada ya uchaguzi huo.
    4
    Mwanamziki wa nyimbo za injili nchini, Christina Shusho akizungumza na waandishi wa habari  kwenye ukumbi wa mikutano uliopo katika ofisi hiyo jijini Dares Salaam kuhusiana na masuala ya amani kuelekea Uchaguzi Mkuu na baada ya uchaguzi huo.
    6
    Baadhi ya waandishi wa habari wakiwa katika mkutano huo.
    ………………………………………………………………….
    Na Magreth Kinabo-maelezo
    Ofisi ya Msajili wa Vyama  Vya Siasa imewaasa na kuwataka viongozi wote wa  vyama  vya siasa kutoa kauli na maelekezo kwa wafuasi wao na wanachama wa vyama vyao kutoshiriki katika aina yoyote ile ya uvunjifu wa amani hususan katika kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu na baada  ya uchaguzi huo.
    Hayo yamesemwa  leo na Msajili wa Vyama Vya Siasa, Jaji Francis Mutungi wakati akizungumza na waandishi wa habari leo kwenye ukumbi wa mikutano uliopo katika ofisi hiyo jijini Dares Salaam.
    "Dhamana  ya nchi iko mikononi mwenu,ushawishi wenu kuhusu amani katika kipindi hiki ndio utakaoliokoa taifa la Tanzania ama  utaliingiza taifa katika vurugu na mfarakano," alisema Jaji Mutungi.
    Jaji Mutungi alisema katika kipindi cha kampeni kumekuwepo na viashiria vya uvunjifu wa amani miongoni mwa jamii yakiwemo baadhi ya makundi ya wanachama, wafuasi na mashabiki wa vyama siasa.
    "Makundi hayo yanadiriki kutoa maneno ya kejeli, matusi, kuvamia, kupigana, hata kujeruhi makundi mengine, ambayo siyo ya upande wao. Hali  iiachwe mara moja ili kuiweka nchi yetu Tanzania  katika hali ya amani na kuiepusha kuingia kwenye vurugu, mfarakano na machafuko yasiyokuwa na  ulazima.
    "Dumisheni amani na kamwe  tusijiingize kwenye siasa zinazoleta mfarakano na uvunjifu wa amani, kumbukeni  kuna maisha baada ya uchaguzi na amani ya nchi yetu ni fahari  yetu sote,alisema  Mutungi.
    Aliongeza ni vyema Watanzania, wakatambua kwamba utofauti wa itikadiya vyama ndio ukomavu wa demokrasia nchini hivyo ni jambo la busara kuvumiliana na kufanya siasa za kiustaarabu.Hivyo  kutovumiliana kwa utofauti wetu wa itikadi za kisiasa kunaweza kulata madhara makubwa kwa jamii itakatopelekea idadi kubwa ya Watanzania kupata athari ikiwemo ulemavu, vifo, ukimbizi,njaa na maradhi.  
    Aidha ofisi hiyo imetoa rai kwa waandishi wa habari watumie kalamu zao vysema kuhubiri amani  na kuepuka kuandika habari za uchochezi, bali wawasaidie wananchi kupata taarifa sahihi zitakazowasaidia kufanya maamuzi wakati wa kuchagua viongozi wao.
    Kwa upande wao mabalozi wa amani, ambao ni Mrisho Mpoto na Christina Shusho walisema kwa nyakati tofauti kuwa wamejitolea kuhubiri amani kupitia fani yao  ili nchi yetu iendelee kuwa na amani.
    Akizungumzia suala hilo, Mpoto aliwapa changamoto waandishi wa habari wajiulize kuwa wana mchango  gani  katika nchi yao ili kuhakikisha inakuwa na amani. Hivyo wanapoandika habari yoyote wakumbuke  kwamba kuna watoto, yatima, walemavu na wajane, isije ikawa ni chanzo cha kuvuruga  amani.
    Naye Shusho alisema kwamba yeye si mfuasi wa chama chochote,bali balozi wa kuhubiri amani.
    Ofisi hiyo imetoa kauli hiyo, kwa kuwa ndiyo yenye jukumu la kuhakikisha ukuaji wa demokrasia unakuwepo kulingana na sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa kikatiba.


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.