MGOMBEA urais wa Tanzania            anayewakilisha Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), Edward            Lowassa amesema hana muda wa kujibu matusi na kejeli            zinazotolewa na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) dhidi            yake.
        Badala yake amesema anatumia muda            uliobaki wa kampeni kutafuta kura kwa wananchi kwa kunadi            ilani ya chama chake. 
        Lowassa aliyeteuliwa na              Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ameeleza hayo              katika mkutano wa kampeni kwenye viwanja vya Mbezi Mwisho,              jimbo la Kibamba, jijini Dar es Salaam.
        Kauli hiyo ameitoa kama mrejesho wa            kampeni ya kimkakati inayofanywa na makada wa CCM walioamua            kumshambulia wakimtuhumu kuwa hafai urais, ni kapi, fisadi na            mgonjwa.
        "Sina muda wa kuwajibu. Tukutane            kwenye sanduku la kura. Katika siku 48 zijazo, mtaamua juu ya            ajira za vijana, afya kama mtaendelea kulala watano watano,            mtaamua juu ya elimu yenu ambayo mimi natamani iwe bure            kuanzia msingi hadi chuo kikuu, maslahi ya walimu na viwanda            vyenye ajira," amesema Lowassa ambaye tangu alipoanza kampeni            amekuwa akiieleza Ilani ya Uchaguzi iliyopitishwa na UKAWA.
        Lowassa amewataka wananchi            kujitokeza kwa wingi kumpigia kura Oktoba 25, na kuzilinda            kura kwa sababu tayari anazo taarifa kuwa CCM wamejipanga            kuiba kura.
        Lowassa alipanda jukwaani
        Viongozi walianza kuhutubia saa            11:38 na kumaliza saa 12:10 jioni huku wananchi wakifika            viwanjani hapo kuanzia saa 4 asubuhi.
        Kulitokea tafrani kidogo pale            viongozi wasimamizi wa jukwaa walipoamua kuwaondoa askari tisa            wa Jeshi la Polisi waliofika mbele ya jukwaa kabla ya viongozi            kwa nia ya kutoa ulinzi. Ilielezwa kuwa viongozi waliona            "polisi hawaaminiki."
        Aidha, Waziri Mkuu mstaafu,            Frederick Sumaye aliyejiunga na Ukawa wiki mbili zilizopita,            amesema CCM hawataki kuachia madaraka licha ya kutokubalika            kwa wananchi kwa sababu ya kudumaza maendeleo na kukumbatia            rushwa na kujikita kumshambulia yeye na Lowassa.
        "Nasisitiza watatoka tu, wamebaki na            kazi ya kumchafua mgombea wetu na mimi. Lowassa alitoka            serikalini miaka minane iliyopita, hata Rais Jakaya Kikwete            alisema lililomkuta ni ajali ya kisiasa na kwamba hakuhusika            na Richmond. Kwa vile leo ametoka CCM anaonekana ni mbaya,"            amesema Sumaye.
        Akihutubia jukwaani, Mwenyekiti wa            Chadema, Freeman Mbowe ameionya CCM na serikali kuacha            kuitumia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuhujumu matokeo ya            uchaguzi mkuu.
        "CCM na serikali wanahofu. Baada ya            kumchafua mgombea wetu pia wana mkakati wa kuitumia TRA            kuingiza bidhaa mfano mafuta bila kulipa ushuru ili kuyauza na            kununulia shahada za kupigia kura," ametuhumu.
        Mgombea ubunge wa jimbo la Kibamba,            John Mnyika alitumia fursa hiyo kujinadi akisema Lowassa            atakapochaguliwa kuwa rais atahakikisha serikali inapeleka            maji jimboni.
        Mnyika ambaye alikuwa mbunge wa            Ubungo, jimbo linalogombaniwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Hali            Halisi Publishers Limited (HHPL), Saed Kubenea, alimtaja            aliyekuwa Katibu Mkuu Chadema, Dk. Willibrod Slaa kuwa sasa ni            adui wa chama hicho.
        Amesema Dk. Slaa baada ya kukaa            kimya kwa zaidi ya mwezi, tangu Chadema kilipomkaribisha            Lowassa kujiunga, ameibuka na kusema chama kimepoteza misingi            yake kwa kumpokea Lowassa na kumteua kugombea urais, hatua            inayoonekana ni ya makusudi ya kuinua CCM.
        "Kuna watu wametoka chooni            wameingizwa chumbani… na mwingine ametoka chumba cha Ukawa na            Chadema ameenda chooni. Tatizo la msingi adui yetu mkubwa ni            CCM. Na sisi tunatangaza atakaeungana na CCM pia ni adui            yetu," amesema Mnyika.
        Kubenea amewataka wananchi            kujitokeza kwa wingi Oktoba 25 kumpigia kura Lowassa huku            wakikumbuka wanapaswa kuondoa maradhi makuu matatu            yaliyotangazwa na Chama cha TANU (Tanganyika African National            Union) ambayo ni maradhi, umasikini na ujinga.
        "Ili Lowassa aweze kufanya kazi            vizuri akiwa rais, lazima tupeleke wabunge wengi wa Ukawa            bungeni. Twende tarehe 25 Oktoba kupiga kura huku tukikumbuka            maneno ya rais mstaafu Benjamin Mkapa aliyekaa madarakani kwa            miaka 10 bila ya kutuondolea upumbavu na ulofa," amesema            Kubenea.
        Mkapa alitoa maneno hayo jukwaani            siku CCM ilipozindua kampeni yake kwenye viwanja vya Jangwani,            Dar es Salaam, alipolenga kumshambulia Sumaye, waziri wake            mkuu wakati alipokuwa rais
        
0 comments:
Post a Comment