Watu watatu wamekufa papo hapo na            wengine wanane kujeruhiwa baada ya bajaj mbili walizokuwa            wakisafiria kugonga lori aina ya Fuso na nyingine kupinduka            katika matukio tofauti mkoani Mbeya.
        Kamanda wa Polisi mkoani Mbeya,            Ahmed Msangi, alisema katika tukio la kwanza, watu wawili            walikufa papo hapo na wengine wanne kujeruhiwa baada ya bajaj            waliyokuwa wakisafiria kugonga lori aina ya Fuso kijiji cha            Hatwelo kata ya Tembela Wilaya ya Mbeya Vijijini. Kamanda            Msangi alisema ajali hiyo ilitokea juzi saa 11:00 jioni.            Aliwataja watu waliopoteza maisha katika ajali hiyo kuwa ni            Abillah Philemon (17), mkazi wa Ilemi jijini Mbeya na Baraka            Seleman (23), mkazi wa Simike jijini hapa.
        Aliitaja bajaj iliyosababisha ajali            hiyo kuwa ni yenye namba za usajili MC 276 APL iliyokuwa            ikiendeshwa na marehemu Philemon ambayo iligonga lori lenye            namba za usajili T588 AMR aina ya Mitsubish Fuso ikiendeshwa            na Emmanuel Francis (35).
        Kamanda Msangi alisema chanzo cha            ajali hiyo ni mwendo kasi wa bajaj.
        "Majeruhi wa ajali hiyo wanatibiwa            katika Hospitali ya Rufaa Mbeya na miili ya marehemu            imehifadhiwa hospitalini hapo," alisema Kamanda Msangi. Katika            ajali ya pili, Kamanda Msangi alisema mtu mmoja mkazi wa            Tewele, Nakonde nchini Zambia, Freddy Ainkala (67), amekufa            papo hapo na wengine wawili kujeruhiwa baada ya bajaj            waliyokuwa wamepanda kuacha njia na kupinduka.
        Kamanda Msangi aliitaja bajaj hiyo            kuwa ni yenye namba za usajili MC 630 AFC iliyokuwa            ikiendeshwa na dereva asiyefahamika na kwamba ajali hiyo            ilitokea juzi saa 9:00 alasiri katika kijiji cha Nkangamo            tarafa ya Ndalambo wilayani Momba. Alisema majeruhi wa ajali            hiyo walipelekwa katika Kituo cha Afya Tunduma kwa matibabu na            mwili wa marehemu Ainkala umehifadhiwa hospitalini hapo.            Aliwataja majeruhi wa ajali hiyo kuwa ni Magreth Ntambo (52)            na Anastazia Nyamungala (55), wakazi wa Kakozi, Nakonde nchini            Zambia.
        Kamanda Msangi alisema chanzo cha            ajali hiyo ni mwendo kasi wa bajaj na kwamba baada ya ajali            kutokea, dereva alikimbia.
        Wakati huo huo, mtu mmoja amekufa            papo hapo na wengine wawili kujeruhiwa baada ya basi la Sai            Baba walilokuwa wakisafiria kugonga lori lililokuwa            limeegeshwa kando kando ya barabara eneo la mlima Nyoka kata            ya Nsaraga jijini Mbeya.
        Kamanda Msangi, alisema kuwa ajali            hiyo ilitokea juzi saa 4:00 usiku wakati basi hilo lenye namba            za usajili T 668 BLD likitokea jijini Dar es Salaam kwenda            Sumbawanga. Kamanda Msangi alisema basi likiwa katika mwendo            wa kasi, liligonga lori lenye namba za usajili T 771 ATV lenye            tela lenye namba za usajili T 771 AUU aina ya Scania            lililokuwa limeharibika na kuegeshwa kando kando ya barabara.
        Alifafanua kuwa aliyepoteza maisha            alikuwa ni utingo wa basi hilo ambaye jina lake halijafahamika            sambamba na majina ya majeruhi hao wawili.
        Kamanda Msangi alisema majeruhi wa            ajali hiyo walipelekwa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya ambako            wanaendelea kupatiwa matibabu na mwili wa marehemu            umehifadhiwa hospitalini hapo.
        Aidha, Kamanda Msangi alisema dereva            wa basi hilo alikimbia baada ya ajali na Jeshi la Polisi            linaendelea kumsaka ili afikishwe mahakamani.
        Kamanda Msangi alitoa wito kwa            madereva kuwa makini waendeshapo vyombo vya moto barabarani            ili kuepuka ajali za kuzuilika.
        
0 comments:
Post a Comment