September 06, 2015

  • Ofa’ ya Makamba yaamsha ‘mabadiliko’ Uwanja wa Taifa



    Ofa' ya Makamba yaamsha 'mabadiliko' Uwanja wa Taifa  Mbunge wa Bumbuli (CCM) January            Makamba.Tukio hilo lilitokea wakati timu ya Taifa ya soka, Taifa Stars ikimenyana na Nigeria kwenye uwanja huo kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika. By Oliver Albert
    Dar es Salaam. Pamoja na Serikali kuzuia kutumia Uwanja wa Taifa kwa shughuli za kisiasa, eneo hilo jana liligeuka uwanja wa kampeni, baada ya mbunge wa Bumbuli (CCM) January Makamba kuruhusu mashabiki walioko nje waingie uwanjani bure.
    Tukio hilo lilitokea wakati timu ya Taifa ya soka, Taifa Stars ikimenyana na Nigeria kwenye uwanja huo kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
    Wakati wa mapumziko, timu ziliporudi vyumbani kwa mapumziko, sauti kutoka kwenye vipaza sauti ilisema: "Mbunge wa Bumbuli, January Makamba, ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM amewaruhusu mashabiki wote walioko nje waingie uwanjani bure.
    Lakini badala ya mashabiki kupokea tangazo hilo kwa shangwe, karibu uwanja mzima ulisimama na kuanza kupiga kelele ukisema "people's power, people's power, people's power" na kunyoosha vidole viwili, ambayo ni alama ya Chadema.
    Baadaye mashabiki hao waliviringisha mikono hewani kuiga ishara inayotumiwa na Chadema na vyama vinavyounda Ukawa kumaanisha mabadiliko.
    Mashabiki hao walianza kulitaja jina la mgombea urais kwa tiketi ya Chadema na Ukawa, Edward Lowassa na kuendelea kufanya hivyo hadi timu zilipokuwa zikirejea uwanjani ndipo wakakaa chini kutazama mchezo.
    Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Makamba alisema Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF) ndilo linaweza kuzungumzia.
    "Sijui chochote labda waulizwe TFF," alisema.
    Msemaji wa TFF, Baraka Kizuguto pia hakutaka kuzungumzia tukio hilo. "Leo ni nafasi ya kocha kuzungumzia mpira wa leo na matokeo," alisema.
    Mashabiki waliohojiwa na Mwananchi walisema watu wamechoshwa na CCM.
    "Watu wamekata tamaa na wanataka mabadiliko," alisema Juma Hamisi, shabiki aliyejitambulisha kuwa anatokea Ukonga baada ya kuulizwa na Mwananchi kuhusu kitendo cha mashabiki kuonyesha waziwazi msimamo wa kisiasa uwanjani hapo.
    "Watu wamechoka kwa kuwa kila mwaka hali ni ile ile. Haijalishi Lowassa ni fisadi au si fisadi watamchagua. "MC alisema watu waingie kwa hisani ya CCM. Hizo ni kampeni za moja kwa moja. Ingekuwa si kipindi cha kampeni wangeruhusu watu waingie bure?"
    Maoni kama hayo yalitolewa na shabiki aliyejitambulisha kwa jina la Anthony Fred wa Tegeta, ambaye alisema watu wameichoka CCM na ndio maana hawataki kusikia lolote kutoka kwao.
    "Kama Makamba alitaka watu waingie bure, angesema tangu jana kabla ya tiketi kuanza kuuzwa. Hizo ni njama za kuwageuza watu akili ili waone CCM inawajali," alisema huku akisisitiza kuwa huu ni mwaka wa mabadiliko.
    Shabiki mwingine aliyejitambulisha kwa jina la Mohamed Hassan alikwenda mbali zaidi na kutabiri kifo cha chama hicho kikongwe.
    "Hali iliyojitokeza uwanjani hapa inaweza kuwa anguko la CCM, hivyo wanatakiwa kujipanga kwa kuwa wana kazi ngumu kwenye uchaguzi wa mwaka huu," alisema.
    Athuman Sadiq, shabiki mwingine aliyekuwapo uwanjani, alisema watu wamezomea kwa sababu walikasirishwa kwa kuwa CCM wameonekana walitaka kutumia mchezo huo kwa ajili ya kampeni.
    Shabiki mwingine, Peter Kisavo wa Mbagala, alisema: "Mimi ni CCM damu, lakini kitendo hiki kimeniudhi, wanataka kutuharibia kuchanganya siasa katika michezo."
    Chadema, ambayo inashirikiana na NCCR-Mageuzi, NLD na CUF kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu, iliomba kutumia uwanja huo wa kisasa wenye uwezo wa kuchukua watu 60,000 kwa ajili ya kufanyia uzinduzi wa kampeni zake, lakini Serikali ikaikatalia kwa maelezo kuwa kwa sasa utumike kwa michezo tu.


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.