June 09, 2014

  • WAZIRI AIBIWA BAADHI YA VITU VYAKE AKIWA GESTI MKOANI SIMIYU



    WAZIRI AIBIWA BAADHI YA VITU VYAKE AKIWA GESTI MKOANI SIMIYU

    Waziri wa Maendeleo  ya  Mifugo  na Uvuvi, Dk  Titus  Kamani,   anadaiwa kuporwa  vitu  mbalimbali zikiwamo   nguo  pamoja  na  fedha, wakati   akiwa  amelala  kwenye   moja  ya  nyumba  za  kulala  wageni  iliyoko  mjini Bariadi  mkoani Simiyu.


    Habari zilizoifikia NIPASHE Jumapili jana zilisema uhalifu huo dhidi ya Waziri ulifanywa  usiku  wa kuamkia  jana.
     
    Akithibitisha  habari hizo  Kamanda  wa  Polisi  mkoani Simiyu, Charles Mkumbo, alisema Dk  Kamani  ambaye  ni mbunge  wa  jimbo  la Busega (CCM) pia Mwenyekiti wa chama hicho mkoani  humo, aliibiwa usiku wa kuamkia jana.
     
    " Ni kweli  tukio  hilo  lipo. Lakini  nipigie simu baadaye  kwa sababu  nipo kwenye  kikao"  alisema  Kamanda  Mkumbo.
     
    Chanzo chetu ndani ya nyumba hiyo kilieleza kuwa vitu  vilivyoibwa  ni pamoja  na nguo, kadi  za benki  na fedha  taslimu, lakini kilikataa kutajwa gazetini.
     
    Inadaiwa  Waziri  huyo  alibaini  kuwapo  kwa wizi  huo  alipoamka  asubuhi,  na hivyo   kutoa  taarifa   katika  kituo  cha polisi  kwa ajili  ya ufuatiliaji.
     
    Jitihada za kumtafuta Dk Kamani  hazikufanikiwa kwa vile  simu  yake japo   iliita kwa muda mrefu lakini haikuwa na majibu.


    CHANZO: NIPASHE JUMAPILI


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.