December 21, 2015

  • Dr. Kigwangalla Ajibu Malalamiko ya Wananchi Kuhusu Sakata la Kuwafungia Watumishi Wachelewaji Geti



    Dr. Kigwangalla Ajibu Malalamiko ya Wananchi Kuhusu Sakata la Kuwafungia Watumishi Wachelewaji Geti
    Ndugu zangu,
    Tunaweza kuibadilisha nchi yetu tukiamua. Wiki iliyopita nili-observe namba ya mahudhurio ofisini na namna watumishi wanavyowasili, nikashangazwa kwamba Waziri wangu, Mhe. Ummy Mwalimu (MB), Katibu Mkuu, CMO - Mganga Mkuu wa Serikali na mimi tunawahi kila siku. Wafanyakazi wenzetu wengi wanachelewa!

    Nikamuomba ruhusa Mkuu wangu wa kazi, Mhe. Ummy, kuwa nichukue hatua. Akanisikiliza akanielewa. Akaniruhusu. Nikatazama sheria inasemaje kuhusu muda wa kuwasili kazini na utaratibu wake wa hatua za kinidhamu. Nikachukua hatua.

    Watu wengi walikasirika. Walikerwa. Kila mtu alisema yake. Najua wengine walichukia. Sawa tu. Lakini wajue ‪#‎HapaKaziTu‬

    Suala hili limezua mjadala mkubwa sana. Wengi wakiitupia lawama serikali wakidai wanaishi maeneo ya mbali na miundombinu ya usafiri siyo mizuri kuwawezesha kuwahi ofisini. Si jambo la kudharau ama la kutokutazamwa, la hasha. Hii ni hoja ya msingi kabisa. Lakini niseme wazi hapa kuwa haishindikani. Ili mimi binafsi niwahi ofisini kwangu saa moja za asubuhi, huamka saa kumi na nusu asubuhi kutokea kule Kijijini kwangu, natakiwa kuvuka Pantoni, na mara nyingi tu hulazimika kuvuka bila gari. Nikifika ng'ambo natembea tu Kwa miguu nawahi ofisini. Namfahamu Mkurugenzi mwingine wa hapa Wizarani, naye hufanya hivyo. Nafahamu Katibu Mkuu wa Wizara naye anaishi Salasala, lakini sijawahi kufika ofisini kabla yake!

    Nidhamu ni tabia. Usipokubali kujituma, mwili unazowea uvivu na uzembe. Na uvivu ni raha. Usipoukataa uvivu hautotoka mwilini. Watanzania wengi wanapenda kuzungumzia Mabadiliko lakini hawataki kubadilika. Tubadilike kwanza sisi wenyewe ndipo tutayaona Mabadiliko tunayoyatamani.

    Kwenye zama za 'Hapa Kazi Tu' viongozi tutakuwa mfano wa Mabadiliko; kwanza, tutawapa wenzetu kwenye utumishi wa umma fursa ya kubadilika, wakishindwa tutawabadilisha!

    Pamoja na hatua hizi za awali za ukaguzi wa kushtukiza, tumeagiza watendaji watazame namna bora zaidi ya kuweka mifumo ya kielektroniki, biometric systems (dole gumba) na kadi za elektroniki, kwenye taasisi zote za Wizara yetu ili kudhibiti mahudhurio ya watumishi na movement yao wakati wote wa kazi. Malengo ni kuboresha huduma kwa wateja wetu.

    Muda wa mwajiri unaibiwa sana. Tutaziba mianya yote mikubwa ya wizi wa muda wa mwajiri.
    Sambamba na mifumo hii, tutaweka utaratibu wa kupima utendaji kazi wa kila mtumishi kwa kuwawekea malengo maalum na kuwapima. Na mfumo huu utakuja sambamba na mfumo wa kutoa motisha Kwa watumishi. Maana hauwezi kumkamua ng'ombe usiyemlisha ipasavyo!

    Ninawapongeza wafanyakazi wote wa Wizara kwa kuwahi mapema leo hii. Mjue tu kuwa sintowaambia ni lini tena tutafunga geti!

    Ahsanteni,
    Dr. Hamisi Kigwangalla, MB.
    Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto.

  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.