Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar              (SMZ) imesema kuwa haina ubavu wa kununua ndege kwa matumizi              ya viongozi wake.
        Waziri wa Fedha Zanzibar, Omary              Yussuf Mzee alisema hayo jana alipojibu swali la mwakilishi              wa Jimbo la Muyuni, Jaku Hashim Ayoub katika kikao cha              Baraza la Wawakilishi.
        Alisema mpango huo unaweza              kufanikiwa baada ya Zanzibar kuanza kuchimba nishati ya              mafuta na gesi.
        Alisema SMZ itaendelea kukodi              ndege kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa              ajili ya matumizi ya viongozi wake.
        Aliwaambia wajumbe wa baraza hilo              kuwa gharama za uendeshaji wa ndege za Serikali ya Muungano              wa Tanzania hutolewa na Serikali ya Muungano, hivyo SMZ              hulazimika kukodi na kulipia gharama.
        "Kuiweka ndege moja Zanzibar ili              itumike kwa viongozi wetu wa kitaifa ni jambo              linalowezekana, lakini kufanya hivyo ni kuongeza gharama za              uendeshaji, kwani wakala watalazimika kuweka vifaa na              wataalamu wa kuzihudumia ndege hizo," alisema Waziri Mzee.
        Awali, mwakilishi huyo alitaka              kufahamu gharama za matumizi ya ndege za Serikali ikiwamo              Foker 50 na 25 zinapotoa huduma SMZ kama zinalipwa na              Serikali ya Muungano au wahisani.
        Pia, mwakilishi huyo alitaka kujua              kwa nini ndege moja isiwe na maskani yake Zanzibar badala ya              kutumika visiwani humo na Tanzania Bara.
        
0 comments:
Post a Comment