Na              Abdallah Juma, Tanga
        Korogwe ni moja kati ya wilaya nane            zinazounda Mkoa wa Tanga. Upande wa Kaskazini, Korogwe            imepakana na Wilaya ya Lushoto, Mashariki kuna Wilaya ya            Muheza, Kusini kuna wilaya ya Handeni na Magharibi kuna Mkoa            wa Kilimanjaro.
        Ndani ya wilaya hiyo, kuna majimbo            mawili ya uchaguzi, likiwemo Korogwe Vijijini linaloongozwa na            Mheshimiwa Stephen Hilary Ngonyani 'Profesa Maji Marefu' kwa            tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).
Wiki iliyopita, Uwazi lilifunga safari mpaka kwenye jimbo hilo ambalo sehemu kubwa ipo milimani na kuzungumza na wananchi wa maeneo mbalimbali ambao walieleza kero mbalimbali zilizokuwa zinawasumbua kisha akatafutwa Mbunge Maji Marefu ambaye alitoa ufafanuzi:
        Wiki iliyopita, Uwazi lilifunga safari mpaka kwenye jimbo hilo ambalo sehemu kubwa ipo milimani na kuzungumza na wananchi wa maeneo mbalimbali ambao walieleza kero mbalimbali zilizokuwa zinawasumbua kisha akatafutwa Mbunge Maji Marefu ambaye alitoa ufafanuzi:
Swali: Mheshimiwa Maji Marefu,            Naitwa Omari Ally, tatizo letu ni kwamba bado barabara za            kuunganisha kati ya Korogwe Mjini na Vijijini ni tatizo hasa            kipindi cha mvua, nyingi ni za changarawe kwa nini usitujengee            lami? Pia kuna Daraja la Mto Rwengela linalounganisha Vijiji            vya Songea na Magoma, mvua ikinyesha kidogo tu maji yanapita            juu, ni lini litafanyiwa marekebisho ili tuondokane na adha            hii?
        Jibu: Wananchi wangu ni mashahidi            kwa jinsi ninavyopigania jimbo letu lipate barabara za lami,            bado mchakato unaendelea na tumefikia hatua nzuri. Hata hizo            za changarawe, nimekuwa wakati mwingine nikitoa fedha zangu            binafsi kwa kushirikiana na halmashauri kuhakikisha            zinafanyiwa ukarabati mara kwa mara. Nyingi zinapitika misimu            yote na hizo chache nazo tunazishughulikia kwa ukamilifu.
        Swali: Naitwa Maimuna Ally, mkazi wa            Kijiji cha Kwetonge. Adha kubwa hapa kijijini kwetu, hatuna            maji ya bomba tunatumia maji ya mito na visima vya wazi ambayo            ni hatari kwa afya zetu na familia zetu. Ni lini na sisi            tutapatiwa huduma ya maji ya bomba kama vijiji vingine?
        Jibu: Maeneo mengi tayari yanapata            huduma ya maji ya bomba na kwa vijiji vichache ambavyo bado,            nawaomba wananchi muwe na subira kwani hii miradi inatekelezwa            kulingana na bajeti ya serikali. Pia maeneo mengine            tunaendelea kuchimba visima.
        Swali: Mheshimiwa mbunge, sisi            wananchi wa Korogwe Vijijini tunaomba tupatiwe ardhi kwenye            mashamba ya mkonge kwani mengi yametelekezwa na wawekezaji na            sisi wananchi hatuna sehemu za kulima, kwa mfano shamba la            Kerenge Mremwa ambalo halifanyi kazi kabisa, tunaomba tugawiwe            wananchi.
        Jibu: Mashamba yote ya mkonge ambayo            hayazalishi, tunafikiria kuwapa wananchi ili wayatumia kwa            uzalishaji wa mazao mengine wakati jitihada za kufufua zao la            mkonge zikiendelea. Wananchi wote wanaoishi jirani na            mashamba, watanufaika baada ya mchakato kukamilika.
        Swali: Mheshimiwa mbunge, naitwa            James Zayumba. Sisi wananchi wa Mombo, Bungu na Magoma kero            yetu kubwa ni katika sekta ya afya. Hospitali ya Mombo na            vituo vya afya vya Bungu na Magoma, kuna wakati ukienda kwa            ajili ya matibabu unaambiwa hakuna dawa tukanunue wenyewe. Je,            ni lini hilo tatizo litaondoka?
        Jibu: Ni kweli kuna tatizo la            upungufu wa dawa kwenye hospitali na vituo vya afya na hili ni            tatizo la nchi nzima. Kwa kushirikiana na serikali na            wafadhili, tunaendelea kulishughulikia na naamini kero hiyo            itaisha kabisa.
        Matatizo mengine yaliyoainishwa na            wananchi wa jimbo hilo, ni uhaba wa walimu hasa wa masomo ya            sayansi na uwindaji haramu katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi            ambapo mbunge huyo amekiri kuyafahamu na kueleza hatua            mbalimbali ambazo anaendelea kuzichukua kwa kushirikiana na            serikali kuu.
        Wiki kadhaa zilizopita, Gazeti hili            lilichapisha kero za wananchi wa Jimbo la Temeke lakini mbunge            wa jimbo hilo, Abbas Mtemvu hakuweza kupatikana kuzijibu.            Jitihada za kumtafuta zinaendelea na atakapopatikana, atatoa            majibu kupitia ukurasa huu- Mhariri.
        Je, umeridhishwa na majibu                ya mbunge wako? Tuma ujumbe mfupi wa maandishi kwenda                namba 0782-398 690 au barua pepe kwa anuani ya                uwazinewspaper@yahoo.com
        
0 comments:
Post a Comment