Mara kadhaa, watu wa              kada mbalimbali wakizungumzia tatizo la ajira nchini, baadhi              ya viongozi wa serikali huwakejeli na kudai kuwa hawana hoja              za msingi.
          Viongozi hao wamekuwa              wakieleza mikakati ya Serikali kuhusu kuwapatia Watanzania              ajira, mipango ambayo kwa kiasi kikuwa ipo katika makaratasi              tu lakini kwa uhalisia hali ni mbaya.
        Nikupe mfano wa mwaka              2006. Utafiti uliofanyika mwaka huo unaonyesha kuwa zaidi ya              asilimia 12 ya vijana nchini hawana ajira na wengi wa vijana              hao wako mijini, yaani asilimia 15 tu ya vijana milioni 25              ndio wenye ajira.
        Asilimia 70 ya vijana              wenye miaka kati ya 13 na 34 ambao ni wengi zaidi kati ya              idadi ya watu milioni 45 waliopo Tanzania ni kundi kubwa              ambalo ni tegemezi na halina ajira na hii ni kati ya nguvu              kazi ya vijana milioni mbili na nusu ambao wako mijini na              hawana ajira.
        Vijana zaidi ya 850,000              wanahitimu masomo kila mwaka huku wakiwa tayari kuingia              kwenye soko la ajira lakini inasikitisha kati ya hao, ni              asilimia 5 ndio wanaopata ajira ya kudumu na asilimia 35              ikijikita katika kilimo ambacho bado kinakabiliwa na              changamoto nyingi zikiwamo zile za uhaba wa pembejeo.
        Hivi sasa vijana zaidi              ya 30,000 wanahitimu katika vyuo mbalimbali na wengi              wakiishia mitaani kutokana na kukosa ajira.
        Hao 30,000 ni wale ambao              walifanikiwa kupenya darasa la saba, kidato cha nne na sita.              Maana yake ni kwamba wapo vijana wengi walioshindwa              kuendelea na masomo kutokana na sababu mbalimbali.
        Wapo walioishia darasa              la saba na kuingia mtaani na wapo walioishia kidato cha nne              na sita na kuishia hukohuko mitaani, huku wakiwa hawana              ujuzi wowote.
        Tatizo la ajira nchini              kwa kiasi kikubwa ni matokeo ya mfumo mbovu wa elimu ambao              unazaa vijana wengi wasio na uwezo wa kuajiriwa popote na              hata kujiajiri.
        Elimu bora inayokidhi              mahitaji ya taifa ndio njia mojawapo na mwafaka ya kutatua              tatizo la ajira nchini kwani fursa za ajira zimejaa duniani              kote na wanaozifaidi ni wale wenye maarifa na ujuzi ambao              msingi wake mkuu unatokana na elimu bora wanayoipata.
        Mfano, nchi yetu haina              vyuo vya ufundi vya kutosha ambavyo vitaweza kuwapokea              vijana walioshindwa kuendelea na sekondari kutokana na              sababu mbalimbali.
        Ni kazi rahisi,              kuanzisha vyuo vya ufundi nchi nzima gharama yake ni              takriban Sh800 bilioni.
          Kama fedha hiyo ni                nyingi unaweza kuwekwa utaratibu katika mafunzo ya Jeshi                la Kujenga Taifa (JKT) ikatolewa elimu ya ufundi na baada                ya mafunzo vijana wapewe vitendea kazi kupitia mikopo                kutoka mifuko ya hifadhi za jamii na kutakiwa kurejesha                baada ya kuanza kuzalisha fedha kupitia shughuli                watakazoanza kuzifanya.
          Kwa sasa hali ni mbaya                kwasababu hata wanaomaliza vyuo vikuu wanakosa maarifa na                asilimia kubwa husubiri kuajiriwa katika nchi ambayo kwa                mwaka inatengeneza ajira kwa kiasi kidogo sana.
          Achilia mbali elimu,                nchi imelala katika sekta ya viwanda wakati sekta hiyo                ndio inayoweza kuajiri watu wa aina yoyote, wenye ujuzi na                wasio na ujuzi, wenye elimu na wasio na elimu,
          Kuimarisha sekta ya                viwanda maana yake ni kuinua sekta ya kilimo ambayo ni                eneo muhimu la kutatua tatizo la ajira. Kwa kujenga uchumi                wa viwanda maana yake utahitaji malighafi ambazo                zinazalishwa hapa nchini.
          Kujenga viwanda vya                kubangua korosho maana yake unawahamasisha wananchi wa                mikoa ya kusini mwa Tanzania kulima kwa wingi korosho                maana unawahakikishia soko la korosho zao.
          Kujenga viwanda vya                kusindika matunda maana yake unawahamasisha wananchi                walime kwa wingi matunda kwa kuwa unawahakikishishia soko                la matunda yao.
          Pia, kujenga viwanda                vya nguo maana yake unawahamasisha wananchi walime                kwawingi pamba kwa kuwa unawahakikishia soko la pamba yao.
          Matokeo yake vijana                wanaodunduliza 'visenti' vyao kufungua biashara zao                kandokando ya barabara kwa lengo la kujipatia riziki,                wanafukuzwa na mabomu ya machozi bila kupewa au kupelekwa                maeneo mbadala watakayoweza kufanyia biashara zao.
          Wakati mwingine                wakipelekwa katika maeneo, aidha yatakuwa hayana                miundombinu au yatakuwa mbali na makazi ya watu.
          Kama serikali haitaki                haya iwekeze kwenye elimu, ijenge uchumi wa viwanda,                ifanye mapinduzi ya kilimo kwani ndio suluhisho la kudumu                la tatizo la ajira nchini.
          Najua kuwa kuna                mikakati ya utekelezaji wa mipango mbalimbali yenye lengo                la kukuza ajira ambayo ni mpango wa mafunzo yenye                kuwezesha vijana kujiajiri, mfuko wa maendeleo ya vijana,                mpango wa kukuza ajira kwa vijana na mpango wa uwezeshaji                wananchi kiuchumi na kukuza ajira.
          Sawa, ila                kinacholalamikiwa na wengi ni kushamiri kwa mipango ya                kwenye makaratasi, mipango ambayo hata ukiambiwa                imetekelezwa haiendani na hali halisi ya maisha ya                Watanzania.
            MWANANCHI.
            
0 comments:
Post a Comment