Suala la uhaba wa dawa              na vifaa tiba katika hospitali nchini ikiwamo Taasisi ya              Saratani ya Ocean Road, limeonekana kuielemea Wizara ya Afya              baada ya Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid              kuthibitisha, huku akidai kuwa Serikali itapeleka fedha kwa              awamu Bohari ya Kuu ya Dawa ili kupunguza uhaba huo.
          Waziri Rashid alikiri              kuwa MSD inaidai Serikali kiasi cha Sh90 bilioni, jambo              ambalo linaifanya bohari hiyo kushindwa kununua dawa kutoka              kwa wauzaji ndani na nje ya nchi. "Ni kweli bohari kuu ya              dawa imepungukiwa fedha za kununulia dawa, lakini siyo kwa              kiasi cha kushindwa kutoa huduma kabisa kama inavyoelezwa.              Kiasi cha pesa kinachotajwa si kigeni na Serikali imekuwa              ikitoa kiasi cha fedha kidogo kidogo ili kuongeza uwezo wa              bohari ya dawa kununua na kusambaza dawa," alisema waziri              katika tamko lake jana.
        Juzi gazeti hili              lilichapisha taarifa ya uhaba wa dawa Taasisi ya ORCI na              kufuatiwa na taarifa kutoka shirika lisilo la kiserikali la              Sikika ambayo ilieleza kuwa Serikali haijalipa kiasi cha              Sh90 bilioni kwa MSD.
        Waziri Rashid alikiri              kuwapo kwa ukosefu wa matibabu OCRI kutokana na uhaba wa              dawa na ubovu wa baadhi ya mashine za mionzi.
        Kadhalika waziri              alionyesha kuwa suala la ORCI ni zito kwa Serikali baada ya              kusema kuwa matibabu katika taasisi hiyo hutolewa bila              malipo.
        "Katika kukabiliana na              hali hii, hospitali zote kupitia waganga wakuu wa mikoa na              wilaya zimeagizwa kupeleka asilimia 50 ya mapato              yanayotokana na uchangiaji kwenda MSD," alisema waziri.
        Alisema wataalamu kutoka              Mpango wa Matokeo Makubwa sasa (BRN) wanamalizia kazi za              utekelezaji wa mpango huo na wamesisitizwa kuzingatia dawa              zinapatikana kwa wakati katika vituo vya matibabu na              kuiboresha MSD.
        Rashid alizitaka              hospitali kuhakikisha zinapeleka asilimia 50 ya mapato licha              ya kuwa wizara inapeleka fedha MSD kwa ajili ya ununuzi wa              dawa na vifaa tiba na kuonya kuwa kiongozi atakayekiuka hilo              atawajibishwa.
        
0 comments:
Post a Comment