Na Mwandishi Maalum,                New York 
        Umoja wa Mataifa                unaitambua Western Sahara kuwa ni Koloni ambalo linapashwa                kuondokana na minyororo ya ukoloni , liwe huru na                lijiamulie mambo yake yenyewe kama taifa huru. 
        Hata hivyo tangu mwaka                1963 Western Sahara ilipotambuliwa kuwa koloni, pamoja na                michakato mbalimbali inayosimamiwa na Umoja wa Mataifa,                Umoja wa Afrika na wadau wengine wengi, bado safari ya                koloni hilo pekee Barani Afrika ya kuikata minyororo ya                ukoloni inazidi kuwa ndefu na yenye mabonde mengi. 
        Kama hiyo haitoshi,                mchakato wa kuisaidia Western Sahara kufikia hatua ya kuwa                nchi huru inaelekea sasa kuigawa Jumuiya ya Kimataifa                katika pande zinazokinzana. 
        Kwa zaidi ya wiki Moja                sasa wajumbe wa Kamati Maalum ya Nne ya Baraza Kuu la                Umoja wa Mataifa inayohusika na Masuala ya Siasa na                Umalizaji wa Ukoloni, wamekuwa wakijadiliana na                kubadilishana mawazo ya namna, pamoja na mambo mengine,                kuchagiza umalizwaji wa ukoloni kwenye makoloni 17                yanayotambuliwa rasmi ndani ya Umoja wa Mataifa ikiwamo                Western Sahara. 
        Ni katika majadaliano                hayo, ambapo pia wajumbe wa Kamati waliwasikiliza                petitioners zaidi ya 60 waliojenga hoja mbalimbali                zikiwamo zinazoitaka Jumuiya ya Kimataifa kwa maana ya                Umoja wa Mataifa kuharakisha mchakato wa kuipatia Western                Sahara uhuru wake kamili au iwe sehemu ya Morocco. 
        Ni katika majadiliano                hayo, ambapo pia, misimamo ya wazi wazi imejitokeza kwa                baadhi ya wajumbe kusimamia au kuegemema upande wa Morocco                ambaye ndiye mtawala ( Mkoloni)wa sasa wa Western Sahara                baada ya mkoloni wa awali Hispania kuliacha mwaka 1963.                Wajumbe wengine zikiwamo nchi za Afrika zinazozungumza                Kiingereza pamoja na nchi za Amerika ya Kati wao zenyewe                zinasimamia katika kutaka Western Sahara iachwe huru na                iwe na haki kuajiamulia hatima yake. Kwa wale wanaogemea                upande wa Morocco, zikiwamo baadhi ya nchi zinazozungumza                Kifaransa nyingi zikiwa za Kiafrika. 
        Wao wanapigia chapuo                hoja inayopendekezwa na Morocco ya kuipatia Western Sahara                uhuru wa kujiamulia baadhi ya mambo yake ( limited                autonomy) lakini ibaki kuwa sehemu kamili ya Morocco. 
         Wanaounga mkono hoja                hii wanaamini kwamba pengine huu ndiyo mwelekeo sahihi wa                kisiasa na wenye kutekelezeka. Lakini wakati huo huo                unakosa hoja ya msingi ya uhuru kamili na kujitawala. Hata                hivyo kundi la pili na ambalo pengine ni kubwa zaidi                lenyewe linapendekeza kuwa wananchi wa Western Sahara na                kwa mujibu wa maazimio ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa                na Baraza Kuu la Usalama wanapashwa kuachiwa wenyewe fursa                ya nini wanataka iwe hatima yao kama ni kuwa na uhuru                kamili nakujiamulia mambo yao au pendekezo hilo la limited                autonomy. 
        Lakini wafanya hivyo                bila ya kushinikizwa na wala wasiamuliwe. Wanaopendekeza                hivyo wanasimamia katika ile misingi inatoainishwa na                katiba ya Umoja wa Mataifa inayowapatia watu wa Saharawi                haki yao ya msingi inayoainishwa katika maazimio                mbalimbali ya Umoja wa yanayowataka wafanye hivyo kupitia                kura ya maoni ( referendum), kama ilivyopendekezwa na                kupitishwa na Baraza Kuu la Usalama kupitia maazimo 658 (                1990) na 690 ( 1991). Hata hivyo pamoja na kupitishwa kwa                maazimio hayo pamoja na kuundwa kwa chombo cha kusimamia                kura hiyo ya maaoni ( MINURSO). 
        Kura hiyo haijafanyika                kutoka na kile kinachoelezwa ni pingamizi zinayowekwa na                Morocco. Jitihada mbalimbali za Mjumbe Maalum wa Katibu                Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Christopher Ross zimeshindwa                kusukuma mbele mchakato wa kuipatia Western Sahara uhuru                wa kujiamulia mambo yake. 
        Kama hiyo haitoshi,                Umoja wa Afrika umemteua Rais mstaafu wa Msumbiji Joachim                Chisano kuwa mjumbe wake maalum wa kulishughulikia suala                la Western Sahara na afanye kazi kwa karibu na Umoja wa                Mataifa. Wajumbe wa Kamati ya Nne wameelezwa kuwa kadri                suala la Western Sahara linavyochelewa kupatiwa ufumbuzi                ndivyo hali inavyozidi kuwa tete hususani katika makambi                ya wakimbizi yanayohudumia wakimbizi wa Western Sahara                wanaohifadhi humo. 
        Wakati wa majadiliano                hayo zilitolewa taarifa zinazoonyesha kuwa katika kambi                hizo za wakimbizi hususani ile ya Tinduff imegeuka au imo                katika hatari ya kugeuzwa eneo ambalo vijana wa Kisaharawi                wanarubuniwa na kuingizwa katika makundi ya ugaidi.                Waliozungumza wanasema vijana hao wameamua kuingia katika                vitendo vya ugaidi kwa kile kinachodaiwa kukata tamaa na                mkwamo wamchakato mzima wa kuamua hatima yao yaani kuwa                huru. 
         Ni kwa sababu hiyo na                tishio hilo la ugaidi katika kambi hizo na mstakabali                mzima wa hali ya Amani na usalama katika eneo la Maghereb,                imefikia wakati sasa ambapo Jumuiya ya Kimataifa                inashauriwa kuliangalia kwa jicho pana zaidi suala la                Western Sahara. 
                Balozi                Ramadhan Mwinyi,  Naibu Muwakilishi wa Kudumu wa  Jamhuri                ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,                akichangia majadiliano  ya jumla kuhusu agenda  ya                umalizaji wa ukoloni katika makoloni 17 yanayotambuliwa                rasmi na Umoja wa Mataifa likiwamo  la Western Sahara                 koloni pekee katika Bara la Afrika. Akizungumza kwa  niaba                ya  Tanzania Balozi Mwinyi pamoja na  mambo mengine                alirejea  wito  Uliotolewa na  Mhe.  Rais Jakaya  Mrisho                Kikwete wakati alipolihutubia Baraza Kuu   la Umoja wa                Mataifa mwezi Septemba, ambapo alilitaka Baraza   Kuu la                Usalama la Umoja wa  Mataifa   kutumia  uwezo wake                kulitafutia ufumbuzi wa kudumu na wa mwisho kuhusu Koloni                hilo la Western  Sahara. Tanzania ni kati ya nchi ambazo                 zimesisitiza haki na uhuru wa  watu wa Saharawi kujiamulia                hatima yake  kwa mujibu wa maazimio na  mapendekezo ya                   Umoja wa Mataifa.  Tanzania licha ya kuwa  mjumbe wa                Kamati ya Nne inayohusika na masuala ya Siasa na Umalizaji                wa Ukoloni  pia ni mjumbe wa  Kamati  ya   nchi 24 ( C24)                ambayo imekasimiwa jukumu la kumaliza ukoloni.
        .jpg)
0 comments:
Post a Comment