July 01, 2014

  • VITAMBULISHO VYA TAIFA KUWAFIKIA LINDI NA MTWARA



    VITAMBULISHO VYA TAIFA KUWAFIKIA LINDI NA MTWARA

     washiriki  katika mkutano wa Wafanyakazi wa  Mamlaka ya vitambulisho vya taifa NIda wakiwa katika picha ya pamoja na mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya arumeru  Munasa  Nyirembe leo nje ya jengo la hotel ya Snowcrest sehemu ambayo mkutano ulikuwa unafanyika 
     Mkurugenzi wa Mamlaka ya vitambulisho vya Taifa (NIDA) , Dickson Maimu akiwa anaongea na waadhishi wa habari kuhusiana na zoezi lima la ugawaji wa kitambulisho cha taifa . 
     washiriki wa  mkutano huo wakiwa wanasikiliza kwa makini mkuu wa wilaya wakati akiongea katika ufunguzi wa mkutano huo 
    ========  ======  ==========
    Na Woinde Shizza,Arusha.
    Mkurugenzi wa Mamlaka ya vitambulisho vya Taifa (NIDA) , Dickson Maimu amesema kuwa zoezi la usajili wa watu na kuwapatia vitambulisho  hivyo litaanza katika mikoa ya Lindi,Mtwara na Pwani  hivi karibuni hivyo amewataka wananchi kutoa ushirikiano ili kufanikisha zoezi hilo.

    Aidha Mkurugenzi huyo amesema kuwa baada ya kukamilisha zoezi hilo katika mikoa ya Dar es Salaam na mikoa yote mitano ya Zanzibar sasa wanaelekea katika mikoa hiyo .

    Akizungumza katika mkutano wa Wafanyakazi wa  Mamlaka hiyo unaoendelea jijini hapa alisema kuwa vitambulisho hivyo vitawasaidia Watanzania kukopesheka kwa urahisi baada ya kutambulika hivyo kuinua kipato cha mtu mmoja mmoja na taifa kwa Ujumla,pia kuwatambua wageni na wakimbizi.

    Maimu amesema kuwa serikali imetenga fedha za kutosha katika bajeti kiasi cha shilingi bilioni  200 ambazo zitasaidia kufanikisha zoezi hilo na kulikamilisha,tunatarajia baada  ya mikoa hiyo itafuata Kilimanjaro,Arusha na Tanga.

    Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arusha ,Nyirembe Munasa alisema kuwa licha ya vitambulisho hivyo kuwasaidia wananchi kiuchumi vitawasaidia katika masuala ya ulinzi na usalama ,kutatusaidia kuwatambua wachafuzi wa amani inawezekana wanatoka nje pia kudhibiti ugaidi.

    Nyirembe ameitaka Mamlaka hiyo kuhakikisha kuwa inatoa elimu ya kutosha kwa wananchi kwa kupitia vyombo vya habari na taasisi mbali mbali zikiwemo shule na vyuo ili watanzania wajue umuhimu wa vitambulisho hivyo .

    Naye Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo kwa upande wa Zanzibar,Vuai Suleman alisema kuwa tayari zoezi hilo limekamilika katika nchi hiyo yenye mikoa 5 na wilaya 10.amewataka watanzania kutoa ushirikiano na kuwa na taarifa muhimu ikiwemo kitambulisho cha mkazi,cheti cha kuzaliwa,vyeti vya kukupigia kura ili kufanikisha zoezi hilo la kitaifa.


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.