December 13, 2014

  • Mstaafu CAG kutuzwa; Aagwa rasmi na Ikulu



    Mstaafu CAG kutuzwa; Aagwa rasmi na Ikulu
    Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Y. Sefue (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mstaafu, Bw. Ludovick Utouh (kulia), na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu mpya wa Hesabu za Serikali, Profesa Mussa Juma Assad (kushoto), katika hafla ya kumpongeza na kumuaga Bw. Utouh iliyofanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency Kilimanjaro jijini Dar es Salaam,11 Desemba, 2014.
    Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Y. Sefue, juzi tarehe 11 Desemba 2014, alimuaga rasmi Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mstaafu Bw. Ludovick Utouh, katika hafla maalum iliyofanyika katika Hoteli ya Hyatt Kilimanjaro jijini Dar es Salaam.
    Hafla hiyo ambayo ilihudhuriwa na baadhi ya Watendaji Wakuu na Waandamizi kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali ilikuwa mahsusi pia kumkaribisha Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu mpya wa Hesabu za Serikali, Profesa Mussa Juma Assad.
    Katika hotuba yake ya kumpongeza Bw. Utouh, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Sefue, alielezea historia ya Utumishi uliotukuka ya Bw. Utouh ambayo imeleta sifa kubwa Ofisi hiyo ndani na nje ya nchi na katika medani za kimataifa. Kwa ujumla, hotuba ya Katibu Mkuu Kiongozi ilijikita kuelezea mchango binafsi wa Bwana Utouh kwa taifa ndani ya miaka zaidi ya arobaini (40) ya Utumishi wake Serikalini.
    Aidha, Katibu Mkuu Kiongozi alielezea mafanikio ya Serikali kwenye eneo la utawala bora, uwajibikaji na uzingatiaji wa sheria, kanuni na taratibu za fedha za umma ambayo yamechangiwa na Bw. Utouh. Balozi Sefue aliwasihi watumishi wa umma kuiga weledi, uaminifu, msimamo, bidii na maarifa ambayo Bw. Utouh alivionyesha kwa vitendo katika utumishi wake.
    Katibu Mkuu Kiongozi alitumia fursa hiyo pia, kumtakia kila la kheri, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali mpya, Profesa Juma Assad, katika kufanikisha majukumu aliyopewa.
    Bwana Utouh alistaafu rasmi nafasi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, tarehe 19 Septemba, 2014 baada ya kuitumikia nafasi hiyo kwa miaka saba na miezi kumi tangu alipoteuliwa na Rais, tarehe 19 Agosti, 2006


  • 0 comments:

    Post a Comment

    Copyright @ 2013 Michapo | Kisiwa cha Habari.